Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM Balozi Seif Ali Iddi alisema Serikali zote mbili zinazosimamia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2010 iliyopata ridhaa ya Wananachi walio wengi kuongoza Dola hazitokubali kuvumilia mtu au Taasisi yoyote inayojaribu kuichezea amani iliyopo Nchini.

Alisema Zanzibar itaendelea kuwa tulivu, amani,salama na Serikali kupitia vyombo vyake vya Ulinzi itakuwa tayari wakati wote kupambana na watu au makundi yoyote yenye muelekeo wa kuhatarisha amani hiyo.

Balozi Seif alitoa kauli hiyo wakati akikabidhi mchango wa Vifaa mbali mbali kwa ajili ya uendelezaji ujenzi wa Maskani ya Chama cha Mapinduzi ya Tupendane iliyopo Kazole ndani ya Jimbo la Kitope.

Alitahadharisha kwamba ye yote atakayejaribu kuleta vurugu au uchochezi ndani ya Zanzibar ahakikishe atashughulikiwa na vyombo vinavyohusika na ulinzi na endapo yupo Mtu au Taasisi inataka kujaribu kutania suala hilo ijaribu kufanya hivyo.

“ Nataka niwahakikishe wananchi kwamba Zanzibar itaendelea kuwa na Utulivu, Zanzibar itakuwa ya Amani. Serikali itakuwa tayari kwa njia ye yote ile kuhakikisha kuwa utulivu wa Jamii unaendeleo kuwepo muda wote ”. Alieleza Balozi Seif.

Akizungumzia suala la Bunge la Katiba linaloendelea Mjini Dodoma Balozi Seif alisema Viongozi wenye nia safi ya Hatma ya Taifa hili watahakikisha kwamba Katiba itakayopatikana italinda maslahi ya Muungano wa Watu wake wa pande zote mbili za Muungano huo.

Aliwathibitishia Wananchi kwamba mchakato wa Bunge hilo la Katiba utakwenda vizuri wakati huuna aliwatahadharisha wananchi kuwa makini katika kufuatilia mchakato huo pamoja na kuwaepuka Viongozi wanaotumia majukwaa ya Kisiasa kujaribu kuwapotosha wananchi kwenye mwenendo wa mchakato huo.

Mjumbe huyo wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM ambae pia ni Mbunge wa Kitope Balozi Seif amewaagiza Vijana wa Maskani hiyo ya CCM ya Tupendane Kazole wajitahidi kumaliza jengo lao haraka iwezekanavyo ili liendane na hadhi ya chama chao.

Balozi Seif pia aliwaomba Vijana hao kuunga mkono wito wa Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Zanzibar ambae pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mh. Dr. Ali Mohd Shein wa kuwataka vijana kufufua maskani za Chama katika maeneo mbali mbali Nchini.

Alieleza kuwa Maskani ndizo jiko na tanuri linalooka watumishi na viongozi Mahiri wa kukisimamia vyema Chama cha Mapinduzi katika utekelezaji wa Ilani na Katiba yake .

Aliwahakikishia Vijana hao wa Maskani ya Tupendane kwamba licha ya Kikao cha bunge Maalum cha Katiba kinachoendelea Mjini Dodoma kujadili Katiba Mpya lakini alisema bado mfumo wa Muungano wa Serikali Mbili Nchini Tanzania ndio wenye nguvu ya kustawisha Umoja na Muungano uliodumu kwa miaka 50 sasa.

Naye Mke wa Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM Mama Asha Suleiman Iddi aliwaasa Vijana hao wa Maskazi ya CCM Tupendane Kazole kuisoma Historia ya Nchihii ili kujaribu kuepuka ushawishi unalenga kuwagawa Vijana hao.

Mapema Balozi Seif alikabidhi vifaa mbali mbali vya ujenzi wa Maskani hiyo ikiwa ni pamoja na Mabati, Miti ya Kuezekea, Matofali, Kokoto, Nondo , saruji pamoja na fedha za Fundi vyote vikiwa na thamani ya shilingi Milioni 1.4.

Naye MamaAsha Suleiman Iddi katika kushajiisha Vijana hao wa Maskani akakabidhi mchango wa Shilingi Laki 400,000/- kwa Vikundi vya Maigizo na Ngoma ili kuwajenga nguvu za uhamasishaji Jimboni humo.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top