Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeombwa kufikiria muundo wa  Miradi mbadala ya Kiuchumi itakayosaidia kutoa ajira, kulinda Mazingira ya Bahari pamoja  na kupunguza msongamano wa wavuvi katika Ghuba ya Chwaka na Marumbi.
Muundo huo wa miradi Mbadala kwa njia nyengine pia utakuwa suluhisho la    kudumu la mgogoro wa muda mrefu wa uvuvi unaokaribia miaka 35 sasa kati ya Vijiji jirani vya Chwaka na Marumbi viliopo Wilaya ya Kati.
Ombi hilo limetolewa na Wananchi wa Kijiji cha Chwaka wakati wakitoa kero pamoja  na changamoto zinazowakabili mbele ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi hapo katika uwanja wa soka wa Chwaka Wilaya ya Kati.
Mkutano huo wa Balozi Seif ni utekelezaji wa ahadi yake aliyoitoa wakati alipokutana na Wananchi wa Marumbi kupokea kero na Matatizo yao miezi michache iliyopita ambayo yanavihusu Vijiji hivyo kwa pamoja kubwa hasa ni suala la Uvuvi.
Bwana  Vuaa Mwadini Mcha alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba idadi kubwa ya Wavuvi wanaofanya shughuli zao za Uvuvi katika ghuba ya Chwaka imekuwa kubwa kulinganisha na uwezo wa ghuba yenyewe.
Hata hivyo Bwana Vuaa alisema Wananchi wa Chwaka wako tayari wakati wowote kumeguka kwa asilimia kubwa kutoka katika shughuli za Uvuvi kama Serikali itaanzisha miradi ya Kiuchumi itakayowawezesha Wananchi hao kujipatia kipato cha kuendesha maisha yao ya kila siku.
“ Tunakumbukumbu nzuri tusiyoisahau ya Rais wa Awamu ya Pili Mzee Aboud Jumbe Mwinyi wakati ule alipotutaka tuachane na uvuvi wa juwa. Kwanza alituwezesha kwa kutuletea nyavu na baadaye taaluma ya matumizi bora ya Bahari mpango ambao ulifanikiwa kwa kiwango kikubwa sana”. Alifafanua Bwana Vuaa Mwadini.
Alimuhakikishia Balozi Seif kwamba Wananchi na Wavuvi wa Chwaka hawana ugomvi na Wananchi wa Marumbi lakini kinachojitokeza  ni Baadhi ya Viongozi wa Serikali na Polisi Wilaya ya Kati kuwa na kigugumizi cha kuchukuwa hatua za kisheria  wakati yanapotokea matatizo hasa ya Uvuvi baina ya pande hizo mbili.
“ Chwaka haiko tayari Mwananchi ye yote  afariki kutokana na ugomvi wa Uvuvi. Lakini tumefikia wakati kukosa  imani dhidi ya  uongozi wa  Polisi na Serikali wa Wilaya ya Kati kwa kushindwa kuchukuwa hatua za kisherika kwa watu  wanaokiuka sheria hizo.
Naye Bwana Nuru Muhammad alielezea masikitiko yao kutokana na Mradi mkubwa ulioanzishwa chini ya uhadhili wa Benki ya Dunia wa kuwawezesha wavuvi wa Ghuba hiyo { Macemp } kutowanufaisha Wavuvi hao ambao ndio walengwa wa mradi huo.
Bwana Nuru alifahamisha kwamba  licha ya juhudi zilizochukuliwa na Wawakilishi wa Mradi huo kupitia wasimamizi wa Benki ya dunia wa kukutana na Wananchi hao kwa kupanga malengo ya mradi huo kiutekelezaji kwa vile mfuko wa mradi huo haukuwa na mashaka lakini kilichojichomoza zaidi kwa mfuko huo ni kuendelezwa kwa semina na vikao.
“ Inasikitisha kuona Vikao mbali mbali vilifanywa kwa kushirikishwa wavuvi husika lakini nguvu za mradi huo zikaelekezwa sehemu nyengine bila ya kuwanufaisha walengwa ambao ni sisi Wavuvi”. Alisisitiza Bwana Nuru.
Akitoa nasaha zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi  alisema wajibu wa Serikali wakati wote ni kufuatilia na kujua kero zinazowakabili Wananchi na kuzitafutia ufumbuzi unaostahiki.
Balozi Seif alielezea kusikitishwa kwake na mgogoro wa uvuvi  unaotia doa mfumo wa amani na utulivu Nchini unaovikumba Vijiji vya Chwaka na Marumbi kwa karibu miaka 35 sasa.
“ Sisi tunataka amani na utulivu, watu waishi pamoja, wafanye kazi pamoja, haya mambo ya Ukafu  na uccm hayana nafasi tena katika Jamii. Tunachokizingatia zaidi kwetu sisi kama Serikali ni kuona wananachi wanaishi kwaamani na  kushirikiana pamoja”. Alisisitiza Balozi Seif.
Katika Mkutano huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliahidi kutoa Mabomba 800  pungufu yaliyooelezwa ndani ya risala ya Wananchi hao wa Chwaka  kukamilisha Mabomba 1200 yaliyokisiwa kutumika katika mradi wa Maji safi na Salama katika Shehia hiyo.
Kwa upande wake Waziri wa Ardhi,  Makazi, Maji na  Nishati Mh. Ramadhan Abdulla  Shaaban aliahidi kugharamia ujenzi wa Tangi la Maji ili kukamilisha mradi huo muhimu.
Hata hivyo  Waziri Shaaban aliwanasihi Wananchi hao wa Chwaka kuwa na stahamala  kidogo kwa vile kazi hiyo inahitaji gharama ambayo kwa hivi sasa  itahitajika kutafutiwa  bajeti yake.
Aliwataka Wananchi hao wa Chwaka kuwa tayari wakati utapowadia       kuitekeleza kazi hiyo  kwa ushirikiano na  Watendaji wa Taasisi za Wizara hiyo kwa njia ya mpango wa ujenzi wa Taifa.
 Othman Khamis Ame  
 Ofisi ya Makamu Pili wa Rais wa Zanzibar     

0 comments:

 
Top