Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzi bar Balozi Seif Ali Iddi alisema Ujenzi wa Taifa imara popote pale hupatikana kutokana na misingi madhubuti inayoandaliwa katika Sekta ya Elimu na kutekelezwa ipasavyo chini ya usimamizi wa walimu.
Kauli hiyo ameitoa katika mahafali ya 10 ya Arusha Modern School kwa wanafunzi wa Maandalizi, Msingi na Sekondari zilizofanyika katika bwalo la Skuli hiyo liliopo Mtaa wa Kisongo nje kidogo ya Mji wa Arusha.
Balozi Seif alisema  msingi huo huwajengea wanafunzi wakati wamalizapo masomo yao uwezo wa kufanyakazi kwa kujiamini wakati wanapoajiriwa katika Taasisi tofauti na hata wale wanaoamuwa kujiajiri wenyewe au kuanzisha Miradi ya Kujitegemea.
“ Lazima mjielewe kwamba nyinyi wanafunzi ni watu muhimu sana katika hatma ya baadaye ya Taifa. Lakini hii haitachipuka tuu bila ya kufanya juhudi za kusaka Elimu itakayokidhi mazingira ya kisasa”. Balozi Seif aliwatanabahisha wanafunzi hao.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwapongeza walimu na wazazi wa Arusha Modern School kwa juhudi zao za pamoja zilizopeleka wanafunzi wa Skuli hiyo kuendelea kufanya vizuri katika mitihani yao ya mwaka.
Balozi Seif alisema  matokeo hayo mazuri yameijengea sifa nzuri skuli hiyo na kuwa miongoni mwa skuli bora kimkoa na hata Kitaifa nchini katika matokeo ya jumla ya kila mwaka.
“Mwaka 2010 darasa la 12 skuli hiyo ilishika nafasi ya 15 Kimkoa na nafasi ya 234 Nchi nzima ,lakini hatimae ikapanda na kufikia nafasi ya pili kimkoa na 38 Nchi nzima kwa mwaka 2011”. Alisisitiza Balozi Seif.
Alieleza kwamba Arusha Medrn School ni moja ya skuli inayoendelea kutoa mchango mkubwa wa elimu katika Taifa kutokana na juhudi zake za kuunga mkono Serikali za kutoa Elimu kwa Kundi kubwa la Vijana ambalo limo katika kujipatia taaluma ndani ya sekta binafsi.
Balozi Seif aliwataka wanafunzi hao kutobweteka na kiwango cha elimu walichokipata na badala yake waongeze juhudi zaidi  katika masomo yao ya ngazi ya juu.
Alisisitiza kwamba thamani ya mwanaadamu katika dunia ya sasa ya sayansi na teknolojia hupimwa kutokana na kiwango chake bora cha elimu alichokuwa nacho.
Akizungumzia suala la wimbi la dawa za kulevya linalooonekana kulikumba kundi kubwa la Vijana Balozi seif  aliwaasa wanafunzi hao kujiepusha na makundi ya kihuni yanayoweza kuwashawishi kujiingiza katika vitendo viovu.
Alisema njia bora ya kupita kwa wanafunzi hao ni kujikita zaidi katika masomo yao pamoja na kufuata ushauri na mafunzowanayopewa na walimu pamoja na wazazi wao.
Katika risala yao wanafunzi hao wa elimu yha Maandalizi, Msingi hadi Sekondari wa Arusha Modern School walisema juhudi za walimu wao zimewawezesha kupelekea kumudu vyema masomo yao hasa katika mfumo wa sasa wa mabadiliko ya Teknolojia.
Wanafunzi hao walielezea furaha yao kutokana na wazazi wao kushuhudia kiwango bora cha elimu ambacho wanaimani kwamba kitawawezesha kuendelea na masomo yao yajayo wakiwa mahiri na kujiamini.
Mapema Mwalimu Mkuu wa Arusha Modern School Bw. Phillip Wasire alieleza kwamba  mafanikio makubwa yaliyopatikana ndani ya skuli hiyo yanatokana na Heshima kubwa yha wanafunzi wao iliyotanguliwa na ushirikiano wa karibu kati ya Wazazi, Uongozi wa Skuli pamoja na Wanafunzi wenyewe.
Bw. Phillip Wasire alisema Uongozi wa Skuli hiyo utahakikisha sifa hiyo ya Heshima iliyojengeka Skulini hapo itaendelea kupewa umuhimu wa kipekee kwa lengo la kuongeza kiwango  bora cha Taaluma.
Katika kutanua wigo wa Taaluma zaidi Mwalimu Mkuu Wasire alifahamisha kwamba uongozi wa Skuli hiyo imefikiria hatua ya kuanzisha masomo ya Uhandisi pamoja na mafunzo ya uendeshaji Ndege ili kuwajengea uwezo  wa ajita wanafunzi hao wakati wanapomaliza masomo yao.
Katika Mahafali hayo  yaliyotawaliwa na burdani tofauti zilizoandaliwa na wanafunzi hao Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alikabidhi vyeti kwa wanafunzi waliomaliza masomo yao ya Maandalizi, Msingi na  Sekondari pamoja na kutoa  zawadi Maalum kwa wanafunzi wa Darasa la 12 na la  14waliopata Daraja la juu katika mitihani yao ya  Taifa.
 Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top