Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema ipo haja kwa jumuiya za Kitaifa na Kimataifa kuendelea kujaribu kuipa msukumo Michezo inayoonekana  kuwa sio  maarufu ili ipate nguvu za ziada kutokana na umuhimu wake ndani ya Jamii.
Alisema michezo imekuwa nyenzo muhimu inayosaidia kuipatia umaarufu Nchi inapoamua kuimarisha  sekta ya michezo na hatimae kupelekea kuongezeka kwa mapato ya Taifa kunakotokana na muingiliano wa wageni kupitia sekta hiyo.
Balozi Seif alieleza hayo hapo Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar mara baada ya kupokea ripoti ya Mpira wa wavu wa Ufukweni Zanzibar { Beach Volley Ball } kutoka kwa Ujumbe wa Chama cha Mchezo huo ukiongozwa na Rais wake Bwana Saleh Salim Saleh.
Amefahamisha kwamba Zanzibar ilibahatika kupata sifa nyingi ndani ya ramani ya Dunia kupitia sekta ya Michezo katika miaka ya nyuma lakini hivi sasa sifa hiyo imetoweka baada ya Michezo kadhaa kufifia na mengine kufa kabisa.
“ Tumeshuhudia enzi zetu wakati tukishiriki michezo tofauti umri ambao tulikuwa maskulini hali iliyopeleka miongoni mwetu kuiiwakilisha Nchi katika michezo ya Kimataifa. Utaratibu huo kwa sasa umetoweka Maskulini sasa tutarajie nini? “. Aliuliza Balozi Seif.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif aliupongeza Uongozi wa Chama cha Mpira wa Wavu wa Ufukweni Zanzibar kwa uwamuzi wake wa kuanzisha Mchezo huo hapa Nchini.
Alisema Mchezo wa Wavu wa Ufukweni unaonekana kupendwa sana na wageni pamoja na Watalii, hivyo kuanzishwa kwake hapa Nchini kutasaidia kwenda sambamba na ile dhana ya Serikali ya kuwa na Mpango wa Utalii kwa wote.
Balozi Seif alitoa wito kwa washirika wa Michezo ndani na nje ya Nchi  kutoa msukumo kwa mchezo huo ili ile azma ya kuanzishwa kwake iweze kufikiwa vyema.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alifahamisha kwamba kwa vile mchezo huo huchezwa zaidi  katika maeneo ya futwe aliutahadharisha Uongozi wa Mahoteli yaliyoko karibu na Fukwe hizo kutowazuia wanamichezo hao kufanya mazoezi yao.
Balozi Seif  alieleza kuwa Vitendo hivyo kama vinafanywa na baadhi ya Mahoteli hayo waelewe kwamba kufanya hivyo ni kwenda kinyume na utaratibu wa matumizi ya fukwe hizo.
“ Upo utaratibu uliowekwa na Serikali kupitia Taasisi ya uwekezaji Vitega uchumi Zanzibar  { ZIPA } kuwataka wawekezaji wote wanaowekeza Vitega Uchumi vyao katika maeneo ya karibu na Bahari kuheshimu Mita 30 za fukwe ili kulinda mazingira”. Alifafanua Balozi Seif.
Akisoma Ripoti hiyo Mwenyekiti  wa Chama wa Mpira wa Wavu wa Ufukweni Zanzibar { ZBV }  Bibi Mwanaisha Saidzain  Abubakar alisema lengo la kuanzishwa kwa mchezo huo  hapa Nchini ni kuitangaza Zanzibar Kitaifa na Kimataifa.
Bibi Mwanaisha aliyataja malengo mengine kuwa ni pamoja na kukuza na kuendeleza michezo, kutafuta vipaji vya wachezaji, kuitangaza Zanzibar kiutalii kupitia mchezo huo pamoja na kubuni ajira kwa Vijana.
Mwenyekiti  huyo wa Chama cha Mpira wa Wavu wa Ufukweni Zanzibar alisema mchezo wao umekuwa ukikabiliwa na changa moto zinazopeleka kuwaweka katika mazingira magumu kimazoezi na hata mashindano.
Bbibi Mwanaisha alizitaja baadhi ya changa moto hizo kuwa ni pamoja na  ukosefu wa viwanja vya mazoezi, Vifaa vya michezo, wafadhili pamoja na ukosefu wa fedha wakati wa kuandaa mashindano yanayokwenda sambamba na utowaji wa elimu.
Naye kwa upande wake Rais wa Chama cha Mchezo wa Wavu wa Ufukweni Bwana Saleh Said  Saleh alimpongeza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwa juhudi zake za kusimamia maendeleo ya Wananchi wa Zanzibar akiwa Mtendaji Mkuu wa Serikali.
Chama cha Mchezo wa Wavu wa Ufukweni Zanzibar {Beach Volley Ball } kimezindua mchezo huo hapa Zanzibar Mwezi Febuari Mwaka huu kwa kuandaa mashindano yaliyoshirikisha  Timu saba za Mchezo huo ambazo zilizojumisha Timu za Vikosi vya Ulinzi na zile za Kiraia.
Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top