Wanachama wa Chama cha Mapinduzi Nchini  wakati wote wanapaswa kuzingatia umadhubuti wa Wanachama wanaowachagua katika kushika nafasi za Uongozi wa Chama hicho kwa nia ya kuhakikisha wanazitetea na kuzilinda Sera pamoja na Ilani ya Chama hicho.
Kauli hiyo imetolewa na Mjumbe wa KAmati Kuu ya Halmashauri Kuuu ya Taifa ya CCM Balozi Seif Ali Idi wakati akiufungua Mkutano Mkuu Maalum wa Uchaguzi wa CCM Wilaya ya Kaskazini B uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Strand iliyoko Kiwengwa Wilaya ya Kaskazini B.
Balozi Seif alisema tabia ya baadhi ya wanachana wa CCM kuchagua Viongozi kwa kuzingatia misingi ya Ujamaa, Ukabila au kujuana inafaa  kuepukwa haraka kwa vile imeshaonyesha ufa ndani ya chama hicho.
Alisema Jahazi la Chama cha Mpainduzi  kuelekea katika harakati za kuimarisha nguvu za chama hicho hasa kwenye uchaguzi Mkuu ujao wa mwaka 2015 lazima liongozwe na manahodha madhubuti watakaokuwa na uwezo wa kuhimili mikikimikiki.
“ Tunataka Viongozi watakaokuwa tayari kutetea kwa nguvu zote  sera na Ilani za chama cha Mapinduzi bila ya kutafuna maneno”. Alisisitiza Balozi Seif.
Balozi Seif ambae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar akiwa pia Mbunge wa Jimbo la Kitope aliwaomba Wanachama na Wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja kukataa kuburuzwa na watu au vikundi vinavyoeneza uchochezi hasa suala muhimu la Maoni ya Katiba Mpya.
Alimpongeza Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja kwa kwa uamuzi wake wa kupiga marufuku mikutano yote inayoashiria cheche ya kuvunjika kwa amani ndani ya Mkoa huo.
Alisema suala la Katiba ipi inafaa kuliongoza Taifa la Tanzania limo ndani ya Maamuzi ya Wananchi wenyewe bila ya kushirikisha maoni au matakwa ya watu, mashirika au Mataifa ya Nje.
Alikumbusha kwamba Sera za Chama cha Mapinduzi zinaendelea kusisitiza Mfumo wa Muungano wa Serikali mbili ambazo faida zake zinaonekana na kila mpenda maendeleo ndani ya Ardhi hii.
Balozi Seif alifahamisha kwamba Muungano uliopo wa Sera za Serikali mbili imeshuhudiwa kupanua harakati za Kiuchumi, Biashara na hata masuala ya Kijamii pamoja na matumizi muhimu ya Ardhi kwa Jamii ya Upande Mmoja wa Muungano huo.
“ Anayesema  Muungano uliopo haufai inafaa Msemaji huyo ajiangalie kwanza na inaonekana wazi kwamba yeye ndie asiyefaa”. Alifafanua Balozi Seif Ali Iddi.
Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Tifa ya CCM aliwapongeza Wana CCM wote  waliojitokeza kuomba nafasi tofauti za Uongozi ndani ya Chama hicho ngazi ya Wilaya.
Balozi Seif alifafanua kwamba majina ya Wanachama yaliyorejeshwa Wilayani Baada ya uchambuzi wa Vikao vya Juu vya Chama hicho yamezingatia vigezo vilivyokubalika ndani ya chama chenyewe ambao ni utaratibu uliowekwa na wanachama wenyewe.
Hata hivyo aliwataka wanachama waliopungukiwa na sifa za uteuzi huo wasikate tama na badala yake waongeze bidii ya kuchapa kazi kwa nia ya kujijengea uwezo wa kuongoza Chama hicho hapo baadaye.
Mapema Katibu wa CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja Bibi Caterine Piter Nao alisema Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Kaskazini B kinatarajia kutoa Tamko rasmi kufuatia  Vitendo vinavyoendelea kutolewa na Baadhi ya Viongozi wa Kisiasa na  Kidini dhidi ya Viongozi wa Juu wa Kitaifa hapa Nchini.
Akitoa shukrani kwa niaba ya Wajumbe wenzake wa Mkutano huo wa Uchaguzi wa CCM Wilaya ya Kaskazini B Mzee Ali Ameir Mohd alisea wapo baadhi ya Viongozi wa Chama hicho wanajaribu kuendeleza tabia za ubabaishaji kitendo ambacho kinafaa kupigwa vita na Wanachama wote wa Chama hicho.
Mzee Ali Ameir alitahadharisha kwamba Kiongozi au Mwanachama yoyote atakayeshindwa kutetea Sera za Chama hicho hafai na anafaa kuepukwa kabisa kuendeleza uozo wake ndani ya chama hicho.
“ Hakuna kazi ndogo ya kulinda Mapinduzi ya Zanzibar. Nitafurahi nikifa hali ya kuwa naendelea kutetea na kulinda sera na ilani ya chama cha Mapinduzi”. Alisisitiza Mzee Ali Ameir Mohd kwa nguvu zake zote.
Mkutano huo Mkuu wa Uchaguzi wa CCM Wilaya ya Kaskazini B. Ulikuwa chini ya usimamizi wa Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa wa Kaskazini Unguja ambae pia ni Mbunge wa Jimbo la Mkwajuni { CCM } Mh. Jadi Simai Jadi.
Othman Khamis  Ame 
 Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar   


0 comments:

 
Top