Rais wa  Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dr. jakaya Mrisho Kiwete alisema Bara la Afrika linaweza kufanikiwa kuondokana na Janga la Umaskini na Njaa endapo Jamii za Mataifa hayo zitajikita zaidi katika kuwa wazi na kushirikiana pamoja.
Rais Kikwete alieleza hayo wakati akiufungua Mkutano wa Pili wa Ushirika wa Mageuzi ya Kijani ya Afrika { African Green Revolution Forum - AGRF  } wa siku tatu unaofanyika katika Ukumbi wa Hoteli ya  Kimataifa ya Ngurdoto Mkoani Arusha ambao pia umehudhuriwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi kwa niaba ya Rais wa Zanzibar Dr. Ali Mohammed Sheni.
Alisema  hakuta kuwa na njia ya mkato kwa Bara hili kuelekea kwenye Kilimo imara bila ya kuwa   na mipango makini itakayosimamiwa na Washirika wa sekta hiyo zikiwemo Taasisi za Umma,Sekta Binafsi na  Jumuiya za kiraia ikitiliwa maanani zaidi Vituo vya Utafiti katika maeneo ya Kilimo hasa Vijijini.
Rais Kikwete alisisitiza kwamba Wakulima wengi ndani ya Bara la Afrika katika maeneo ya Vijijini wanakabiliwa na Taaluma duni inayochangia kudumaza uzalishaji katiika sekta ya Kilimo.
Alifahamisha kwamba jembe la mkono linaloendelea kutumiwa na Wakulima walio wengi  Barani Afrika linapunguza nguvu za Wakulima hao katika uzalishaji na hatimae kuzindisha matatizo na mapungufu katika Sekta hiyo muhimu.
“ Nguvu nyingi za Wakulima wadogo wadogo Barani Afrika zinaishia katika jembe la Mkono ambalo hutumiwa na wakulima waliowengi hasa Vijijini”. Alisisitiza Rais Kikwete.
Alieleza kuwa Kilimo kinaendelea kuwa chanzo kikubwa cha utajiri wa Afrika licha ya kuwa sera ambazo hazikuhitaji na kutiliwa maanani  katika miongo kadhaa iliyopita.
Hata hivyo alifafanua kwamba Kilimo kitaendelea kuwa msingi wa usalama wa chakula na maendeleo ya Kiuchumi.
Aidha alieleza kuwa dhamira iliyopo ya pamoja iliyojumuisha makundi mbali mbali ya sekta ya Umma na zile Binafsi katika  Mkutano huo wa Pili wa Ushirika wa Mageuzi ya Kijani Barani Afrika  inaweza kushawishi muelekeo wa mageuzi na uwekezaji kwenye Kilimo cha Bara la Afrika.
Alisema Kilimo kinaajiri zaidi ya asilimia 65% ya nguvu kazi Barani Afrika na kinaendelea kuongoza uchumi wa Mataifa mengi ya Bara hili ikiwa ni kati ya asilimia 60% na 80% ya mapato ya ndani.
Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania aliupongeza Uongozi wa Ushirika wa Mageuzi ya Kijani ya Afrika { AGRF } kwa uamuzi wake wa kuufanya Mkutano huo wa Pili Nchini Tanzania uamuzi ambao umeipa heshima kubwa Tanzania katika Nyanja za Kimataifa.
Kupitia Mkutano huo Rais Kikwete pia alimpongeza Mwenyekiti mwenza ambaye pia ni muanzilishi wa Mfuko wa Kimataifa wa Misaada Bibi Melinda Gates kwa juhudi zake za kuendelea kuunga mkono harakati za Kiuchumi na Kijamii za Mataifa maskini Duniani ikiwemo Tanzania.
Naye Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akitoa salamu katika Mkutano huo kwa niaba ya Rais wa Zanzibar Dr. Ali Mohammed Sheni alisema mkazo unaendelea kuchukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuwajengea uwezo Wakulima Wadogo wadogo.
Balozi Seif alisema  Mkazo huo umewekwa kupitia msaada wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo ya Kilimo { IFAD } sambamba na uimarishwaji wa Kituo cha Utafiti wa Kilimo kiliopo  Kizimbani.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alieleza kuwa   Zanzibar bado imekipa Kilimo kipaumbele  katika kumkomboa Mwananchi ambapo zaidi ya asilimia 80% ya watu wote wanategemea Kilimo ambacho ni sekta muhimili  kwa Uchumi na Maendeleo ya Taifa.
Mapema  Mwenyekiti wa Ushirika wa Mageuzi ya Kijani ya Afrika ambaye pia ni Katibu Mkuu Mstaafu wa Umojwa Mataifa Dr. Koffi Annan alisema Afrika inahitaji kuongeza nguvu katika kuwajengea uwezo wa uzalishaji Wakulima wadogo wadogo hasa kutokana na asilimia 60% ya Ardhi ya Bara hili kuwa ni jangwa.
Dr. Annan alisema  ni vyema Wataalamu wakaangalia zaidi mbinu bora za kuimarisha miundo mbinu katika maeneo ya Vijijini ili kupambana na changamoto zilizopo kwa kutumia mbinu za kisasa za Kilimo.
“ Mafanikio ya Bara la Afrika katika kutanuka Kiuchumi kutategemea miundo mbinu ya uwekezaji katika maeneo ya wakulima wadogo wadogo hasa Vijijini”. Alisisitiza Mwenyekiti huyo wa Ushirika wa Mageuzi ya Kijani ya Afrika { AGRF } Dr. Annan.
Aliongeza kwamba mbinu hizo ni vyema zikaenda  sambamba na ushirikishwaji wa Sekta Binafsi pamoja na uendelezwaji wa Sekta ya utunzaji wa Mazingira.
Kwa upande wake Mwenyekiti Mwenza ambae pia ni muanzilishi wa wa Mfuko wa Kimataifa wa Misaada Bibi Melinda Gates ameipongeza Tanzania kwa hatua yake ya kuimarisha Sekta ya Kilimo kupitia Mpango wake wa Kilimo kwanza.
Aliahidi kwamba Taasisi yake itaendelea kuunga mkono jitihada za Mataifa kadhaa ulimwenguni katika harakati zao za kujikwamua na umaskini na kuondokana na maradhi.
Mkutano huo wa Pili wa Ushirika wa Mageuzi ya Kijani ya Afrika { AGRF } umehudhuriwa na Washiriki zaidi ya elfu moja kutoka Taasisi, Jumuiya na Mashirika mbali mbali ya ndani na nje ya Bara la Afrika.
 Othman Khamis Ame              
  Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
                                                                           

0 comments:

 
Top