Utekelezaji wa kazi za Chama Cha Mapinduzi { CCM } utakuwa rahisi iwapo Viongozi wapya wa Umoja wa Vijana wa CCM watajipanga vyema katika kutekeleza majukumu yao watayopewa kwa mujibu wa katiba na Sera za Chama hicho.
Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya CCM Wilaya ya Kaskazini “B”  Mama Asha Suleiman Iddi alieleza hayo wakati akiufungua Mkutano Mkuu wa Uchaguzi wa Umoja wa Vijana wa CCM Wilaya  hiyo uliofanyika katika Ofisi ya CCM Jimbo la Kitope uliopo Kinduni Wilayani humo.
Mama Asha alisema bila ya Vijana hao kujituma ipasavyo Chama chao hakitakuwa na uwezo wa kupiga hatua za haraka za Maendeleo ambayo ndio nguvu itakayokiwezesha kujijengea uzoefu wa ushindi katika chaguzi zote zijazo.
Aliwataka Vijana hao kusimama kidete  katika kuwakataa Watu wanaogombea uongozi wakiwa na sura mbili hata kama  watu hao watatumia uwezo wao wa kifedha.
“ Wakati wa kuyakataa mapandikizi ndani ya chaguzi zetu kipindi hichi umefika. Lazima tuyapembue mapumba yanayotukorofisha na tuwe makini katika kuchagua Viongozi wenye uchungu na Nchi”. Alitahadharisha Mama Asha Suleiman Iddi.
Mama Asha aliwaomba Wanachama hao wa Umoja wa Vijana wa CCM kutowarejesha madarakani Viongozi wa chama hicho ambao tayari wameshaonyesha nia ya kuzipinda sera za Chama chao.
Alifahamisha kwamba Wapo baadhi ya Viongozi, Watu na hata Vikundi vya Kidini vinavyotaka Nchi hii isitawalike kwa kueneza kasumba ya kupinga kila linalotakiwa na kupangwa na  Serikali.
“ Tayari tumeshakuwa na Amani, Utulivu na maelewano ndani ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inayofuata mfumo wa Umoja wa Kitaifa. Sasa inakuaje tena kunajitokeza kasumba zisizoeleweka mwanzo wala mwisho wake?”. Aliuliza Mama Asha.
Mjumbe huyo wa Kamati ya Siasa ya Wilaya ya Kaskazini “B” aliupongeza Uongozi uliopita wa Umoja huo wa Vijana wa CCM ambao umekiwezesha Chama cha Mapinduzi na Jumuiya zake ndani ya Wilaya hiyo kufikia hatua makini ya utekelezaji wa sera zake.
Mapema Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM Wilaya ya Kaskazini “B” Ndugu Ali Khamis Ali alisema uchaguzi wa Umoja huo ngazi za Matawi na Majimbo umekwenda vyema kama ulivyokadiriwa.
Ndugu Ali alisema umefika wakati kwa Wanachama wa Umoja huo kuwachaguwa Viongozi wazuri zaidi ya wote ambao waliomba nafasi za kuuongoza Umoja huo.
“ Ni furaha ilioje kwa Vijana hao ambao ndio majeshi ya Chama cha Mapinduzi kumaliza chaguzi hizo kwa ufanisi wa hali ya juu”. Alifafanua Katibu wa UVCCM wa Wilaya hiyo.
Kwa upande wake akitoa shukrani zake baada ya ufunguzi wa Mkutano huo wa Uchaguzi wa UVCCM Kamanda wa Vijana wa Wilaya ya Kaskazini B Ndugu Khamis Salum Ali alieleza kwamba Uomja huo utahakikisha unaisaidia Serikali Kuu katika utekelezaji wa Sera za Chama cha Mapinduzi zilizopata ridhaa ya Wananchi na kupelekea kuingia madarakani.
Nd. Khamis alisema moja ya Sera zilizomo ndani ya chama hicho ni kusimamia suala la amani na utulivu ambayo inaonekana kuanza kuchezewa na baadhi ya Watu na hata vikundi vya Dini.
“ Ukweli hatutakuwa tayari kuona amani yetu iliyomo ndani ya Wilaya na Mkoa wetu  wa Kaskazini wanakuja watu kutaka kuichezea. Kwa hili tutaonekana wabaya”. Alitahadharisha Kamanda huyo wa UVCCM Wilaya ya Kaskazini “B”.
 Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top