Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iko tayari kuwasaidia Vijana waliotengemaa baada ya kuacha matumizi ya dawa za kulevya kwa kuwapatia mtaji endapo vijana hao wataamaua kubuni na hatimae kuanzisha miradi ya kujiimarisha Kiuchumi.
Kauli hiyo imetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wakati akizungumza na Viongozi na baadhi ya Vijana waliomo ndani ya nyumba saba za kurekebishia tabia Unguja kwa watu waliokuwa  wakitumia  dawa za kulevya hapo katika moja ya nyumba hizo iliyopo Mtaa wa Nyarugusu Shehia ya Pangawe Wilaya ya Magharibi.
Balozi Seif alisema Serikali kupitia Wizara inayosimamia masuala ya Ajira ina mpango wa kuwawezesha Wananchi hasa Vijana kujiendesha kimaisha  katika dhana nzima ya kuwajengea mazingira ya kuchapa kazi kwa vile Vijana ndio nguvu kazi kubwa inayotegemewa na Taifa.
Alisema kazi kubwa inaendelea kufanywa kupitia Taasisi, Jumuiya Washirika wa Maendeleo kwa kushirikiana na Serikali  ya kubadilisha tabia kwa Watu na hasa Vijana kuacha kuendelea kutumia dawa za kulevya.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alizinasihi Familia zenye Vijana wanaotumia au kuathirika na matumizi ya dawa hizo kuacha hulka ya kuwatenga Vijana wao jambo ambalo linaweza kuwazidishia kutumbukia katika janga hilo kwa kukosa ushauri pamoja na msaada.
Balozi Seif alisema katika kukabiliana na tatizo hilo ni vyema kwa Familia hizo kujenga tabia ya kufuatilia kwa kina Vijana wao walioko katika Nyumba za Kurekebisha Tabia kwa lengo la kuwarejesha katika mazingira yao ya kawaida.
Aliwapongeza Vijana hao walioamua kuacha matumizi ya dawa za kulevya kwa hiari yao na kuwataka wahakikishe wanajilinda kwa nguvu zao zote kuwepuka kurejea katika matumizi hayo hatari kwa afya zao.
Alisema vitendo hivyo walivyokuwa wakivifanya kabla vimewasababishia kupungukiwa na akili, Maarifa na hata nguvu kazi zao zilizokuwa zikitegemewa na familia pamoja na Taifa kwa ujumla.
“ Tusipokuwa na hadhari Taifa linaweza kuangamia kwa kukosa nguvu kazi ya Vijana hasa kwa kuzingatia kuwa takwimu zilizopo zinaeleza kuwa wengi wa Vijana waliotumia dawa za kulevya wameathirika na maambukizi ya Virusi vya Ukimwi. Sasa hii ni balaa”. Alitahadharisha Balozi Seif.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alishauri ipo haja kwa Jamii kwa kushirikiana na Serikali Kuu pamoja na washirika wa Maendeleo kutafuta mbinu za kuwajengea mazingira bora Vijana walioacha matumizi ya dawa hizo ili wajiepushe kurejea katika magenge ya kihuni.
Mapema Mlezi Mkuu wa Nyumba saba za kurekebishia Watu wanaotumia dawa za kulevya Zanzibar Bibi Fatma Sukwa alisema asilimia  42% ya watu waliopitia katika Nyumba hizo wameacha matumizi ya Dawa za kulevya katika kipindi cha miaka mitatu.
Bibi Fatma alifafanua kwamba asilimia 48% ya Vijana waliopitia Nyumba hizo wamerejea kutumia dawa za kulevya baada ya kutengwa na Familia zao, asilimia 1% hadi sasa hawajuilikani taarifa zao tokea waondoke katika Nyumba hizo.
Mshauri huyo Mkuu wa Nyumba za kurekebishia tabia kwa watu waliotumia dawa za kulevya ameitahadharisha Jamii kuelewa kwamba dawa za kulevya ni ugonjwa kama magonjwa mengine yanayowazunguuka wanaadamu.
Kwa upande wake Mshauri wa kuacha dawa za kulevya na kubadilisha tabia katika nyumba saba za kurekebishia tabia za Unguja na Pemba Bwana Ahmed Islam alisema Jamii inapaswa kuacha tabia ya kuwanyooshea vidole Vijana walioathirika kutokana na matumizi ya dawa za kulevya.
Bwana Ahmed Islamu alimpongeza na kumshukuru Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif kwa msaada wake ambao ni faraja kwao ukionyesha kuyathamini makundi hayo ya Vijana  .
Katika ziara na Mkutano huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alikabidhi msaada wa Baskeli kwa Kijana Mlemavu Sabri Ameir Issa ili iweze kumrahisishia harakati zake za kimaisha.
Shughuli hiyo pia ilikwenda sambamba na Viongozi na Vijana hao wa nyumba za kurekebishia tabia kukabidhiwa msaada wa vyakula kwa ajili ya matumizi yao ya kila siku.
Balozi Seif alikabidhi Msaada huo kwa Mshauri Mkuu wa Nyumba hizo za kurekebishia watu walioathirika na matumizi ya dawa za kulevya Bibi Fatma Sukwa.
Othman Khamis  Ame 
 Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar                   

0 comments:

 
Top