Taasisi inayoshughulikia Taaluma ya Teknolojia ya Afya ya chuo Kikuu cha Brown Mjini Boston Nchini Marekani { Med International } imelenga kuisaidia Zanzibar katika Sekta ya Afya ili kufikia kiwango kinachokubalika         Kiteknolojia.
Kauli hiyo imetolewa na Mkurugenzi Mwenza wa Taasisi hiyo Bwana  Han Shen Chia wakati akikabidhi Ripoti ya utafiti wa Afya uliofanywa na Wataalamu wa Taasisi hiyo katika Hospitali za Unguja na Pemba.
Bwana Han Shen akiwa pamoja na Mwakilishi na Mkurugenzi wa Taasisi hiyo ya Med International  Bwana Jayson Marwaha alisema utafiti huo uliochukuwa takriban wiki 10 umejaribu kutoa hali halisi ya mapungufu na maeneo ambayo Taasisi yao inaweza kusaidia kitaaluma  na hata uwezeshaji.
“ Faraja ilioje na la kutia moyo kuona baadhi ya vitengo vya uchunguzi wa matumbo { utra sound } na sehemu za kuhifadhia watoto wachanga wanaozaliwa kabla ya kufikia muda wake vinatoa huduma kwa asilimia   100%”. Alisema Mkurugenzi huyo mwenza wa Med Inaternational Bwana Han.
Alisema Mipango inaendelea kuimarishwa ili kuona Taasisi hiyo inawatumia Wataalamu wa Sekta hiyo kuja kutoa mafunzo kwa Walimu wa Afya hapa Zanzibar.
Bwana Han alifahamisha kwamba utaratibu wa kuwapata wataalamu hao hasa wakati wa kipindi cha joto ambacho wanakuwa mapumziko utazingatiwa zaidi.
Kwa upande wake Mwakilishi na Mkurugenzi wa Med International Bwana Jayson Marwaha alimueleza Balozi Seif kwamba utafiti wao kwa kuanzia utaangalia zaidi kuimarisha Hospitali za Mnazi Mmoja Unguja na ya Chake Chake Pemba.
Bwana Marwaha alisema mpango huo utafuatiwa pia na Taasisi za Nchi hiyo kuweka vitega uchumi vyao vya Sekta ya Afya hapo baadaye katika Visiwa vya Zanzibar.
Alifahamisha kwamba uwekezaji huo utazingatia na kutegemea Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itakavyoridhia mapendekezo yaliyomo kwenye ripoti hiyo.
Akitoa shukrani zake kwa hatua za Uongozi wa Taasisi hiyo ya Med Inaternational katika kusaidia sekta ya Afya Zanzibar Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema juhudi za Taasisi hiyo zimeanza kuonyesha mwanga wa matumaini katika sekta hiyo muhimu kwa Jamii.
Balozi Seif aliuambia Ujumbe huo wa Med Inaternational kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar bado ina azma ya kuzijengea uwezo Hospiotali zake za rufaa ili zitoe huduma katika kiwango kinachokubalika kitaalamu zaidi.
Alisema hospitali Kuu za hapa Zanzibar bado zinahitaji nguvu zaidi kufikia lengo hilo. Hivyo ushiriki wa Taasisi hizo washirika wa maendeleo unaweza kwa kiasi kikubwa kuongeza kasi ya uimarishaji huo.
“ Nimeanza kupata matumaini makubwa  ya ujio wenu hapa Zanzibar kufuatia ziara yangu ya mwezi oktoba mwaka jana nchini Marekani. Hata wenzetu wa Chuo Kikuu cha Florida Nchini humo tunaendelea kuwasiliana nao ambao nao mwaka jana tulitiliana saini mkataba wa ushirikiano na chuo chetu Kikuu cha Taifa Zanzibar { SUZA }”. Alifafanua Balozi Seif.
Wataalamu wa Taasisi hiyo inayoshughulikia Taaluma ya Teknolojia ya Afya ya Chuo Kikuu cha Brown Mjini Boston Nchini Marekani kwa kushirikiana na Watendaji wa Wizara ya Afya Zanzibar wamemaliza utafiti wao kabla ya muda waliojipangia wa Tarehe 2/9/2012.
 Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top