MAKAMU WA PILI WA RAIS WA ZANZIBAR BALOZI SEIF ALI IDDI AKISALIMIANA NA KATIBU MKUU WA MIKUTANO YA KIMATAIFA YA UKANDA WA MAZIWA MAKUU BALOZI LIBERETE MULAMULA ALIYEIKA OFISINI KWAKE VUGA MJINI ZANZIBAR
Viongozi wa Mataifa yaliyomo ndani ya Ukanda ya Maziwa Makuu Barani Afrika wana wajibu mkubwa wa kuhakikisha amani iliyorudi ndani ya ukanda huo inaendelea kuwepo na kulindwa kwa nguvu zote.
Katibu mkuu wa Mikutano ya Ukanda huo Balozi Liberata Mulamula alieleza hayo wakati akizungumza na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi hapo Afisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.
Balozi Mulamula alisema Jumuiya ya Afrika ya Mashariki hivi sasa imefikia pahala pazuri katika kuelekea kwenye maendeleo baada ya muda mrefu wa vurugu na migogoro ya vita vya wenyewe kwa wenyewe katika Baadhi ya Mataifa ya Jumuiya Hiyo.Balozi Mulamula alisema kwamba huu ni muda muwafaka kwa jamii za Mataifa ya Ukanda huu kuelekeza nguvu zao katika uzalishaji mali kwa vile eneo hili bado lina Rasilmali nyingi ambazo mpaka sasa hazija tumika.
“ Tunashukuru kwamba hali ya Ukanda wa Maziwa Makuu imetulia kidogo, hivyo ni vyema tukaichunga chunga isipotee ”. Alisema Balozi Mulamula.
Aliipongeza Tanzania kupitia Vaiongozi wake wa Awamu mbali mbali kwa juhudi zake za kusaidia amani ndani ya Ukanda huu jambo ambalo limeleta faraja kwa jamii nyingi hivi sasa. Naye Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Balozi Mulamula anastahiki kuheshimiwa na Mataifa ya Ukanda huu kwa juhudi zake zilizosaidia kusukuma kasi ya amani ndani ya kanda hii. Alisema bado wapo watu wenye mawazo ya kutaka yaliyotokea Rwanda, Burundi na Somalia yatokee pia kwenye Mataifa yenye am,ani ndani ya Ukanda wa Maziwa Makuu.
“ Wenzetu wanatusema kuwa Afrika ni mahala pa Njaa, Umaskini na Mapigano lakini wanasahau kwamba mengine wanasababisha na kuyasimamia wao ”. Alisisitiza Balozi Seif.
Wakati huo huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Amepokea Mchango wa pole ulotolewa na Wananchi wa Mkoa wa Tanga kwa ajili ya Mfuko wa Maafa Zanzibar.
Mchango huo umewasilishwa na Mkuu wa Mkoa huo Luten Mstaafu Chiku Gallawa akiuongoza ujumbe wa Viongozi sita wakiwemo pia wafanyabiashara wa Mkoa huo. Luteni Mstaafu Chiku Gallawa alisema wana Tanga wa haki ya kuwafariji wenzao wa Zanzibar kwa vile jamii za Wananchi wake zimeingiliana kidamu.
Alisisitiza haja ya kufanya kazi pamoja katika kahakikisha sheria na taratibu za mwenendo mzima wa usafiri wa Baharini ambao pia unaunganisha maeneo hayo mawili unazingatiwa vyema.
Kwa upande wake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ameushukuru Uongozi huo pamoja na Wananchi wa Mkoa wa Tanga kwa kuonyesha kuguswa kwao na Msiba uliowakumba wenzao wa Zanzibar wa Kuzama kwa Meli ya M.V.Spice Islanders Tarahe 10 mwezi Septemba mwaka huu.
Uongozi wa Mkoa wa Tanga Umekabidhi Mchango wa zaidi ya Shilingi Milioni kumi na Moja Nukta Mbili.
Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top