Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kutoa Taaluma kwa Jamii juu ya namna ya kumlinda mototo na majanga yanayotokana na udhalilishwaji wa kijinsia ili wakue katika mazingira bora Kiafya.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ametoa kauli hiyo hapo katika ukumbi wa Zanzibar Beach Resort wakati akizindua Mpango Mtambuka wa kumjenga Mtoto wa Zanzibar.
Balozi Seif alisema udhalilishaji wa Watoto Kitaifa na Kimataifa bado unatisha na juhudi za pamoja inafaa kuchukuliwa kwa lengo la kukabiliana na tatizo hilo.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisisitiza kwamba Serikali haitomfumbia macho mtu ye yoye atakayebainika anamdhalilisha motto.
‘ Naendelea kusisitiza kwamba Mtu yeyote atakayehukumiwa kwa kosa la udhalilishaji wa Watoto au Wanawake Kijinsia atawekwa hadharani upitia vyombo vya Habari ili Jamii itambue uovu wake ”. Alisema Balozi Seif.
Aliziomba Taasisi na Mashirika ya Kijamii kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuweka mikakati ya kukabiliana na wimbi hili la Udhalilishaji.
Alisema Takwimu za Shirika la Afya Ulimwenguni WHO za mwaka 2001 zinaonyesha Watoto wa Kike 150 Milioni na 73 Milioni Wanaume wameathirika kisaikolojia baada ya kudhalilishwa Kijinsia.
Balozi Seif amezipongeza Taasisi za Serikali, Binafsi na Mashirika na Nchi wahisani kwa mchango wao wa kusaidia makuzi ya Mtoto hapa Zanzibar.
Mapema Balozi wa Umoja wa Ulaya Bwana Tim Clarke alisema bado utumikishwaji wa Watoto katika Sekta za Uchukuzi, Ujenzi, Ukahaba na kazi ndogo ndogo Majumbani unaonekana kuendelezwa na baadhi ya Watu.
Balozi Clark alisema si vyema kuona ajira kandamizi dhidi ya Watoto wadogo zinaendelezwa Jambo ambalo lonawanyima Haki yao ya msingi ya Elimu.
Naye Balozi wa Sweden Nchini Tanzania Bwana Lennarth Hjelmaker alitanabahisha kwamba ni vyema kwa Serikali na Jamii zote kuhakikisha kwamba Mabadiliko ya Makuzi ya Watoto yanalindwa .
Balozi Lennarth alisema hatua hiyo ikizingatiwa inaweza kusaidia kupunguza au kuondosha matamanio na tamaa za Watu wanaopenda kudhalilisha watoto.
Uzinduzi wa Mpango Mtambuka wa kumjenga Mtoto wa Zanzibar umeshirikisha pia Wataalamu wa Mashirika na Taasisi mbali mbali za Ndani na Nje ya Nchi.
Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top