TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Urasimu unaoendelea kuwepo ambao huwapata wananchi wanaoomba mashamba ya mikarafuu yaliyokosa huduma ya kuyaendeleza umeelezwa kuwa unachangia kudumaza uzalishaji wa zao la karafuu katika shehia kadhaa Kisiwani Pemba.
Kauli hiyo imetolewa na baadhi ya masheha mbele ya kamati Maalum ya kushughulikia mashamba ya Serikali iliyo chini ya mwenyekiti wake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi iliyo Kisiwani Pemba kuratibu Mashamba yote ya Serikali.
Masheha hao wamesema mashamba mengi ndani ya shehia zao ambayo yako katika umiliki wa Serikali na hata zile eka tatu tatu zilizokosa umiliki baada ya wenyewe kufariki yamekosa huduma ya uendelezwaji.
Wameeleza kuwa ukosefu huo wa huduma umepelekea mikarafuu mingi kupotea kwa kuzongwa na misitu.
“ Kwa kweli mashamba yaliyoachwa bila ya huduma yanadhoofisha uzalishaji” Amesema Bw. Othman Shehe sheha wa shehia ya chonga chake chake. Akiwashukuru Masheha hao kwa ushirikiano wao na Viongozi wa Serikali Mwenyekiti wa Kamati Maalum ya Kuratibu Mashamba ya Serikali ambaye pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amesema adha ya kuomba omba hupungua iwapo Taifa litakuwa na udhibiti mzuri wa Uchumi wake .Balozi Seif amesema si jambo zuri kuona zao la karafuu ambalo ni uchumi wa Taifa linauzwa kiholela kinyume na utaratibu nje ya Zanzibar.
“ Batra yote tuliyonayo katika uchumi wetu inatokana na zao la karafuu ”.Alisema Balozi Seif Iddi.Amefahamisha kwamba lengo la Serikali kuu ni kuona zao la Karafuu linaimarika kwa vile tayari soko lake liko katika kiwango kikubwa kimataifa.
Amesema Masheha bado wana wajibu wa kuhamasisha wananchi wao juu suala zima la kuliimarisha zao hilo ili kwenda sambamba na lile lengo la serikali kuu.  “ Hakikisheni hakuna uchafu wowote unaotokea katika shehia zenu kuhusu zao la karafuu” Amefahamisha Balozi Seif.
Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top