Na Jumbe Ismailly-Ikungi
ZOEZI la uzinduzi wa uchangiaji wa damu salama lililozinduliwa kiwilaya katika kata ya Minyughe,tarafa ya Ihanja,Mkoani Singida limepokelewa na wananchi wa kata hiyo kwa hisia tofauti kutokana na baadhi yao kuamini kuwa endapo watatoa damu upo uwezekano wa kupata madhara katika siku za baadaye. 

Uzinduzi huo uliofanyika katika Kijiji cha Minyughe unalenga kupunguza vifo vya akina mama wakati wa kujifungua katika wilaya ya Ikungi na Mkoa wa Singida kwa ujumla. 

Mjumbe wa serikali ya Kijiji cha Minyughe,George Mahuna aliyasema hayo alipokuwa akizungumzia hofu ya zoezi hilo kufanikiwa katika upatikanaji wa damu nyingi kwa ajili ya kuwasaidia wagonjwa wanaokwenda katika vituo vya kutolea huduma za afya kufuata matibabu mbalimbali. 

“Kwa ukweli zoezi hili la utoaji wa damu hapa Kijijini kwetu na katika kata yetu ya Minyughe jambo hili ni jipya na mara ya kwanza limepokelewa kwa hisia tofauti tofauti,kwa sababu ni jambo jipya kumekuwa na maneno mengine ya kupotosha”alifafanua mjumbe huyo wa serikali ya Kijiji cha Minyughe. 

Kwa mujibu wa Mahona baadhi ya wananchi wamekuwa wakipotoshwa kwamba zoezi hilo la uchangiaji damu limekuwa likigubikwa na imani za jamii ya freemason,na licha ya wengine kulipokea vizuri lakini bado wanahofu kubwa miongoni mwao kutokana na sababu mbali mbali. 

“Bado wanahofu kwa sababu hili ni jambo geni kabisa katika kata hii na katika Kijiji hiki,kwa hiyo wamekuwa na wasiwasi unapotoa damu huwenda baadaye unaweza ukapata madhara katika afya kwa hiyo hili limekuwa ni tatizo sana”alisisitiza Mahona. 

Hata hivyo mjumbe huyo wa serikali ya Kijiji aliweka bayana kwamba ili kuondokana na hali hiyo zoezi la uchangiaji hup wa damu Halina budi kufanyika mara kwa mara ili waweze kulizoea ili ule uzushi na woga uweze kuwatoka kabisa na waone ni jambo la kawaida kwa wao kuchangia damu kwa hiyari na kuokoa maisha ya wagonjwa. 

Alibainisha Mahona kwamba mpaka sasa wananchi hawana elimu kabisa juu ya faida ya kuchangia damu salama na kutoa mfano kuwa hata yeye ambaye anayeonekana kuwa ni mwelewa,lakini bado hana elimu hiyo. 

“Elimu ya kutosha hakuna,hata mimi ninayezungumza hapa ni mara yangu ya kwanza na nimefika hapa ili nijifunze na kupata elimu juu ya jambo hilo kwa hali hiyo bado kuna umuhimu kwa wananchi hao kupatiwa elimu juu ya jambo hili ili waondokane na dhana hiyo potofu”alisisitiza Mahona. 

Naye mkazi wa Kijiji cha Minyughe,Mwajabu Pamba alitaka kufahamu serikali imejipangaje kumsaidia mama mjamzito anapopelekwa kwenye kituo cha afya kwenda kujifungua unatakiwa uwe na mipira ya kukusaidia kujifungua,wakati mumewe hana uwezo wa kifedha kugharamia vifaa hivyo?”alihoji Mwajabu.

Awali akimkaribisha kuzindua uchangiaji wa damu salama katika viwanja vya shule ya msingi Minyughe,Mganga Mkuu wa wilaya ya Ikungi,Dk.Christopher Ntamakanya alisema sababu kubwa ya vifo vinavyotokea takribani asilimia kati ya 26 au robo ya wananwake wanaojifungua katika vituo vya kutolea huduma inatokana na kuvuja damu nyingi. 

“Sababu ziko nyingi sana,lakini leo nazungumzia moja tu ambayo inahusiana na akina mama waiawazito,”alisema 

Aliweka wazi daktari huyo kwamba wilaya ya Ikungi inapoteza idadi kubwa ya akina mama wajawazito wanaopata ujauzito kabla ya kujifungua au baada ya kujifungua. 

“Lakini takribani asilimia 26 au robo ya akina mama wanaojifungua inatokana na kuvuja damu nyingi hasa damu hii inavuja wakati tofauti tofauti,kuna wakati inavuja kabla ya kujifungua,na wakati mwingine inavuja baada ya kujifungua”alifafanua. 

Awali akizindua uchangiaji wa damu salama,Mfuko wa afya ya jamii(CHF) na daftari la ufuatiliaji akina mama wajawazito,Mkuu wa wilaya ya Ikungi,Miraji Mtaturu alisema wilaya hiyo imekuwa na idadi kubwa ya vifo vya akina mama wanaojifungua inayoongezeka mwaka hadi mwaka.

0 comments:

 
Top