Na: Khamis Haji, Milan Italy
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, amefungua milango kwa wafanyabiashra na wawekezaji wa Ulaya kutumia fursa nzuri za uzalishaji wa biashara za viungo na utalii nchini ili kuweza kufungua miradi yao.

Amesema kwa miaka mingi Zanzibar imejulikana kama visiwa vya viungo (Spice Islands) kutokana na utajiri mkubwa wa mazao hayo, hali ambayo imechangia kukua kwa soko la utalii na kuimarisha uchumi wake.

Maalim Seif amesema hayo alipokuwa akihutubia katika maadhimisho ya siku ya Tanzania, kwenye maonyesho ya kibiashara ya kimataifa yanayofanyika mjini Milan Italy, ambapo zaidi ya nchi 140 zinashiriki.

Amesema sekta ya kilimo cha viungo kama karafuu na bidhaa nyengine zinazozalishwa Zanzibar na Tanzania Bara, ni eneo linaloweza kupewa kipaumbele na wafanyabiashara hao na kuweza kuwanufaisha wananchi wa Tanzania ambao wengi wao ni wakulima.

Katika sekta ya utalii Maalim Seif ambaye anamuwakilisha Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano kwenye maonyesho hayo amesema, vivutio vilivyopo Tanzania ikiwemo Mji Mkongwe wa Zanzibar, Mlima Kilimanjaro, mbuga za wanayama na fukwe, imeifanya Tanzania kuwa nchi ya kipekee.

“Tanzania tuna utajiri mkubwa wa rasilimali, tunayo gesi na mafuta, madini mbali mbali ikiwemo Tanzanite, mazingira bora kwa kilimo na vivutio vya utalii. Nakuombeni tumieni fursa hizi kuja kuwekeza”, amesema Maalim Seif.

Ameishukuru Serikali ya Italy kwa kuandaa maonyesho hayo na kuifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi washiriki, na kwamba kitendo hicho kinadhihirisha uhusiano mwema uliopo kati ya Italii na Tanzania.

Mapema akizungumza kwenye maonyesho hayo, Mkurugenzi Mkuu wa maonyesho hayo ya Milan 2015 Bw. Bruno Antonio Pasquino ameelezea kuridhishwa na ushiriki wa Tanzania kwenye maonyesho hayo, pamoja mazingira mazuri ya uwekezaji.

Amesema ushiriki huo ni fursa nzuri kwa Tanzania kuweza kujitangaza kwa mataifa mbali mbali yanayoshiriki maonyesho hayo, ili hatimaye wawekezaji waweze kuvutika na kuelekeza miradi yao nchini Tanzania.

Naye Mkurugenzi wa banda la maonyesho la Tanzania bibi Twilumba Mlelwa amesema bidhaa za kitanzania zilizopo kwenye maonyesho hayo zikiwemo za viungo na sanaa, zimekuwa kivutio kikubwa kwa wageni.

Maalim Seif pia alipata fursa ya kutembelea mabanda ya nchi mbali mbali kwenye maonyesho hayo zikiwemo wenyeji Italia na Kazakstan ambayo inatarajiwa kuandaa maonyesho kama hayo mwaka 2017, pamoja na kutembelea mabanda yote ya nchi za Afrika Mashariki.

Maonyesho hayo yalipambwa kwa burudani maalum ya ngoma iliyochezwa na kikundi cha sanaa cha Bagamoyo.

0 comments:

 
Top