Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seis Ali Iddi alisema kwamba Taasisi za kidini zina mchango muhimu katika malezi ya vijana katika kuepuka mambo mabaya na kutilia mkazo mambo mema ili kuwaandaa kwenye maisha yao ya sasa na yale ya baadae. 

Alisema jamii inapaswa kuendelea kutumia fursa za mafundisho ya dini kukemea tabia na mienendo inayopelekea vijana hao wasijiingize kwenye mambo yanayokwenda kinyume na maamrisho ya dini.

Balozi alieleza hayo kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr.Ali Mohamed Shein katika uzinduzi wa Kongamano la kumuenzi mwanafalsafa wa fani ya Kihistoria Ulimwenguni Dr. David Livingstone lililoandaliwa na Kanisa la Anglikana Zanzibar na kufanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Grand Palace Kinu cha Taa Malindi Mjini Zanzibar.

Alisema ni jambo la kutia moyo kuona kuwa jitihada kubwa zinafanyika miongoni mwa taasisi za kidini hapa nchini, lakini ni vyema taasisi hizo kwa kushirikiana na waumini wao na wananchi kwa jumla wakaongeza nguvu kukabiliana na changamoto inaendelea kuwaathiri vijana ambao ndio nguvu kazi ya Taifa kila uchao.

“ Tuendelee kuwafundisha vijana pamoja na watoto wetu ili wajiepushe na hatari zinazowakabili katika maisha yao ya kila siku hasa yale maambukizo ya virusi vya UKIMWI na athari za matumizi ya dawa za kulevya “ Alifafanua Balozi Seif

Balozi Seif aliipongeza Jumuiya ya Marafiki wa Dr. David Livingstone { FDDL } kwa utaratibu wao wa kufanya maadhimisho ya miaka 141 tokea kukomeshwa kwa biashara ya utumwa hapa Zanzibar.

Alisema hatua hiyo ni utaratibu mzuri unaotokana na nafasi ya Zanzibar kuwa kitovu cha ziara za wageni wengi kupitia visiwa vya Zanzibar katika ziara za wageni hao ndani ya mwambao wa Afrika Mashariki na Kati, kama ilivyokuwa kwa Mmishionari David Livingstone aliyepita Zanzibar mwaka 1853 na 1856.

“ Nimefurahi kusikia kuwa utaratibu huu wa kufanya maadhimisho haya kila mwaka ni wa kupokezana ambapo mwaka 2013 ilikuwa zamu ya wenzetu wa Bagamoyo na mwaka huu hapa Zanzibar. Hali hii inadhihirisha kuwepo kwa uhusiano mkubwa wa kihistori baina ya wananzhi wa Tanzania Bara na Zanzibar “. Alisisitiza Balozi Seif.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwaomba washiriki wa kongamano hilo kuyatumia maarifa na uzoefu watakaoupata kutokana na maisha ya Dr. David Livingstone katika kuwatumikia wanaadamu wenzao ili na jamii ya sasa iwe na moyo wa kuwatumikia wengine.

Aliwapongeza viongozi wa dini na madhehebu mbali mbali nchini kwa kutekeleza wajibu wao wa kuwaongoza waumini wao katika misingi ya imani inayozingatia kuheshimiana, kuvumiliana, utiifu wa sheria na kuendeleza hali ya amani na utulivu nchini.

Alisema taasisi za Kidini zina mchango mkubwa katika malezi ya vijana ili kuwaandaa kwenye maisha yao ya sasa na baadaye kwa vile dinin zote zinakataza mabaya na kutilia mkazo matendo mema.

Balozi Seif aliwahimiza Viongozi kuendelea kutumia fursa za mafundisho ya dini kukemea tabia na mienendo inayopelekea vijana wengi kutojiingiza kwenye mambo yanayokwenda kinyume na maamrisho ya Dini.

“ Tuendelee kuwafundisha watoto wetu ili wajiepushe na hatari ya maambukizo ya virusi vya ukimwi na athari za matumizi ya dawa za kulevya “. Alisisitiza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.

Balozi Seif alieleza kwamba ni jambo la kutia moyo kuona kwamba jitihada kubwa zinafanyika miongoni mwa taasisi za kidini, lakini ni vyema taasisi hizo zikajitahidi kuongeza nguvu ili kupambana na changamoto zinazowapata vijana.

Akizungumza suala la huduma za Kijamii Balozi Seif alizopongeza Taasisi za Kidini Nchini kwa juhudi zao za kuiunga mkono Serikali katika kuwapatia huduma za kijamii wananchi katika maeneo mbali mbali Nchini.

Alisema idadi ya skuli binafsi zinazomilikiwa na taasisi za kidini nchini zimefikia 20 wakati vituo vy afya vya taasisi hizo vimekuwa vikiongezeka kila siku hatua ambayo inaisaidia Serikali katika kuwaondoshea usumbufu wa kupata huduma hizo muhimu wananchi.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alitoa wito kwa kwa taasisi za kidini kuendelea na jitihada zao katika suala la kuwatunza wazee na watoto wanaoishi katika mazingira magumu.

Alisema hatua hiyo itakwenda sambamba na mipango ya Serikali katika kufanikisha lengo la kluwaandaa raia na waumini wema wenye elimu bora, afya nzuri mambo ambayo ni msingi imara katika kuendeleza ustawi wa jamii.

Katika ufunguzi wa Kongamano hilo la kumuenzi Dr. David Livingstone Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif pia alikabidhi vyeti maalum kwa watu mashuhuri kutokana na mchango wao uliofanikisha utaratibu huo.

Mapema Mwenyekiti wa Jumuiya ya Marafiki wa Dr. David Livingstone { FDDL } Lous Majaliwa alisema lengo la kuanzishwa kwa jumuiya yake ni kuendeleza mchango mkubwa alioutowa Mwafalsafa huyo wa masuala ya Kihistoria ulimwenguni.

Bwana Majaliwa alisema Dr. David livingstone ataendelea kukumbukwa kutokana na jitihada zake za kusimamia mpango wa kutokomeza utumwa ndani ya ukanda wa bara la Aafrika.

“ Tmeshuhudia katika historia Dr. David Livingstone alitumwa na serikali yake ya Uingereza kuja Afrika kati kati ya karne ya 18 kufanya utafiti wa mto nile na kukuta tatizo kubwa zaidi la biashara ya utumwa afrika mashariki ”. Alisema mwenyekiti huyo wa FDDL.

Alisema uchungu alioupata Dr. David kutokana na madhila waliyokuwa wakifanyiwa watumwa ulimfanya kurudi tena Afrika kufanya kampeni ya kutokomeza biashara ya utumwa hali ambayo ilifanikiwa tarehe 6 june mwaka 1873 mwezi mmoja tuu baada ya kufariki kwake.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Mkamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top