Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Seif Ali Iddi ameonya kuzuiwa kufanywa kwa ujenzi wa aina wowote katika eneo la Masoko makongwe liliopo Mtaa wa Selemu ndani ya Mji wa Wete hadi Serikali Kuu itakapotoa maamuzi yake.

Balozi Seif alitoa onyo hilo mara baada ya kuliangalia eneo hilo lililoleta mgogoro baina ya Uongozi wa Baraza la Mji Wete pamoja na Wafanyabiashara wa soko hilo dhidi ya mfanyabiashara Ahmed Abdulla Mapete aliyeuziwa sehemu hiyo na baadhi ya watendaji wa Baraza la Mji Wete kinyume na taratibu za Serikali.

Alisema Serikali ilitenga eneo hilo maalum kwa ajili ya huduma za soko ili litoe huduma kwa wakaazi wa Mji huo tokea mwaka 1942. Hivyo amewaagiza wafanyabiashara wanaoendesha biashara zao katika sehemu hiyo waendelee kama kawaida hadi Serikali Kuu itakapotoa maamuzi kutokana na mgogoro huo.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alimekea vitendo vya baadhi ya watumishi wa umma wanaoamua kujichukulia maamuzi mikononi mwao kinyume na taratibu zilizowekwa na Serikali na hatua za kuwawajibisha hazitochelea kuwachukulia dhidi ya watumishi hao.

“ Hili ni soko lililotengwa na Serikali kwa ajili ya kuwajengea mazingira wananachi kupata huduma za msingi za mahitaji yao ya kila siku. Sasa hii tabia ya baadhi ya watendaji kujichukulia maamuzi kwa kuzitelekeza mali za Serikali wamepewa amri na nani ? “ Alikemea Balozi Seif.

Balozi Seif alisema kwamba mtu ye yote atakayeamua kuuza eneo la Serikali bila ya idhini ya Taasisi inayohusika na masuala ya ardhi aelewe kwamba anafanya makosa na Serikali haitakuwa tayari kulipa fidia endapo mali au jengo aliloiweka katika ardhi hiyo itaondoshwa.

Alifahamisha kwamba mgogoro wa soko kongwe la Selemu Wete tayari unaeleweka Serikalini na muda si mrefu maamuzi rasmi ya suala hilo la muda mrefu yatatolewa kwa mujibu wa sheria na taratibu za Serikali.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top