Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ameiagiza Serikali ya Mkoa wa Kaskazini Pemba kufanya tathmini mara moja nyumba zote zilizoathirika kutokana na moto mkubwa uliokikumba Kijiji cha Shumba Mjini leo majira ya saa 5.00 za asubuhi.

Nyumba zipatazo 14 zikiwa na wakaazi 100 zimeathirika vibaya kutokana na moto huo na nyengine 24 kuezuliwa mapaa yake kwa hofu ya kuathirika na moto huo ambao hadi sasa kwa mujibu wa taarifa za Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kaskazini Pemba Shehani Mohd Shehani kwamba chanzo chake bado hakijafahamika huku uchunguzi wa jeshi la polisi pamoja na vikosi vyengine vya ulnzi ukiendelea.

Balozi Seif ambae pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Maafa Zanzibar akiwa kisiwani Pemba kwa shughuli mbali mbali za Maadhimisho ya Miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar alitoa agizo hilo muda mfupi baada ya kuwafariji wananchi wa Kijiji cha Shumba Mjini kutokana na maafa waliyoyapata ya janga la moto.

Akiwapa pole wananchi hao 100 waliohifadhiwa kwenye madrasa mmoja Kijijini humo na baadaye kupelekwa Skuli ya Kijiji hicho Balozi Seif aliwataka kuwa na subra katika kipindi hichi cha mitihani na Serikali inajipanga kuangalia namna ya kuwasaidia wananchi hao.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaandaa kikao maalum cha dharura keshokutwa jumatatu ili kulijadili suala hili na kuona jinsi itakavyoweza kukusanya nguvu za kuwasaidia wananchi walioathirika na janga hili.

“ Wakati nimeshamuagiza Mkuu wenu wa Mkoa kufanya tathmini ya janga hili mimi kama mtendaji Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na vile vile nikiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Maafa Zanzibar nitawajibika kuitisha kikao cha dharuura Jumatatu kulitafakari suala hilo “. Alisema Balozi Seif.

Alisisitiza kwamba ni wajibu wa Serikali Kuu kutafuta mbinu na utaratibu utakaoweza kutoa fursa nzuri ya kujaribu kusaidiana Wananchi walioathirika na Maafa hayo.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwashukuru wananachi na baadhi ya Taasisi zilizojitokeza kwa njia mbali mbali kusaidia wananchi hao ikiwemo vyakula, vifaa na baadhi ya huduma muhimu kama nguo kwa wale wananchi 100 waliokuwa wakiishi kwenye zile nyumba 14 zilizounguwa na kuteketeza vitu mbali mbali.

Aidha Balozi Seif aliupongeza Uongozi wa Wilaya ya Micheweni pamoja na Mkoa wa Kaskazini Pemba kwa hatua iliyochukuwa ya kuandaa mazingira ya kuwahifadhi wale wananachi watakaokosa hifadhi na kuwapeleka katika Skuli ya Kijiji hicho cha Shumba Mjini.

Akitoa shukrani kwa niaba ya Wananci wa Kijiji cha Shumba Mjini Mwakilishi wa Jimbo la Micheweni Mh. Subeit Juma Khamis amempongeza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif kwa hatua aliyochukuwa ya kuwafariji wananchi hao katika muda mfupi baada ya kutokea tukio hilo.

Mh. Subeit alimuelezea Balozi Seif kuwa ni kiongozi mwenye moyo unaomuelekeza kujali wananchi wake.

Moto huo mkubwa uliokuwa ukivuma kutokana na upepo mkali licha ya taarifa za awali za kutotambulikana chanzo chake ulianzia kwenye Nyumba ya Bwana Masoud Ali Khamis na naadhi ya wananchi walisikika wakisema chanzo chake kimesababishwa na watoto waliokuwa wakijiandaa kupika mlo wa mchana.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top