Mamlaka ya maeneo huru ya uwekezaji ya Hamriya Nchini Sharja imeonyesha nia ya kutaka kujenga kikwanda kikubwa Zanzibar cha usafishaji wa mafuta ya vyombo vya moto na Baharini kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na kuongeza mapato ya pande hizo mbili rafiki.

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa uhifadhi wa mazingira ambae pia ni mshauri wa maendeleo ya ujenzi wa Mamlaka hiyo Dr. Mohammad Tariq wakati akizungumza na Ujumbe wa Zanzibar unaoongozwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ukiwa ziarani Dubai ulipopata fursa ya kutembelea miradi kadhaa maendeleo iliyomo maeneo huru ya uwekezaji ndani ya Mamlaka hiyo.

Dr. Mohammad aliuelezea ujumbe huo wa Zanzibar kwamba Uongozi wa Mamlaka hiyo umeamua kujenga kiwanda hicho ili kitoe huduma za mafuta sambamba na kujaribu kudhibiti upandaji holela wa mafuta katika mwambao wote wa Afrika Mashariki.

“ Uwezo wa kuuza mafuta chini ya thamani ya shilingi 1,500/- kwa lita unawezekana kama tunaweza kujenga kiwanda hicho hivi sasa Zanzibar kutokana na utafiti tuliofanya wa bidhaa hiyo kimataifa “. Alifafanua Dr. Mohammad.

Alisema Kampuni maarufu za Kimataifa zilizo chini ya Mamlaka hiyo za ALCO Group na ABS zimekuwa na uwezo mkubwa wa kusafirisha na kusafirisha bidhaa hiyo kwa kutumia mashine na meli zake popote pale wanapopata tenda.

Dr. Mohammad alifahamisha kwamba Kampuni hizo zimekuwa zikipokea mali ghafi ya mafuta kutoka Oman kwa huyasafisha na baadaye kuyasafirisha Nchi mbali mbali yakiwa tayari kwa matumizi ya vyombo.

“ Bandari yetu Maarufu ya Amriya imekuwa ikipokea mali ghafi ya mafuta, tunayasafisha na hatimaye tani zisizopungua 90,000 husafirishwa nchi tofauti duniani zikiwemo Marekani na Australia “. Alifafanua Dr. Mohammad.

Dr. Mohammad alieleza kuwa Mamlaka hiyo imeliangalia soko la Zanzibar na kunaona kwamba inaweza kufanya Biashara kwa kuingia ubia na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa vile uwezo wa Kampuni zake wa kuzalisha mafuta unafikia Tani 500 kwa siku ukikadiriwa kufikia faida kati ya Dola za Kimarekani Milioni 80 na 90.

Naye Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif ameihakikishia Mamlaka hiyo ya Maeneo huru ya Uwekezaji ya Hamriya ya Nchini Sharja kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iko tayari kushirikiana na Makampuni hayo katika harakati zake za kutaka kuanzisha kiwanda cha usafishaji wa mafuta.

Balozi Seif alisema fursa kama hiyo ya uwekezaji ambayo imekuwa ikitafutwa kwa muda wote na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itasaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha uchumi na mapato ya pande zote mbili.

Alieleza kwamba Zanzibar imekuwa katika harakati za kuimarisha miundo mbinu ya Bara bara, Umeme, Maji na Mawasiliano ili kuwajengea mazingira mazuri wawekezaji wanaofikia maamuzi ya kutaka kuwekeza Vitege uchumi Visiwani Zanzibar.

“ Kwa mradi huu mkubwa ambao sote ni mashahidi utakaosaidia pia ajira kwa vijana wetu sisi hatuna vikwazo vyovyote tunachokuombeni nyinyi washirika wetu muharakishe kuandika maombi yenu ili tuone namna gani tunaweza kufikia hatua nzuri ya ushirikiano wa kuanzisha mradi huo “. Alieleza Balozi Seif.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar katika ziara hiyo alitembelea Kampuni ya uzalishaji wa Mafuta ya ALCO na ABS, kuona maendeleo ya utanuzi wa bandari ya Hamriya, Eneo la matengenezo la Vyombo vya Baharini { Chelezo } lililo chini ya uendeshaji wa Kampuni ya Kimataifa ya Damen na Nchini Uholanzi.

Baadaye balozi Seif na Ujumbe wake alikagua harakati za uzalishaji katika Kiwanda cha kutengeneza nondo kinachopata mali ghafi za kokoto kutoka Mkoani Tanga Tanzania.

Eneo huru la uwekezaji la Mamlaka ya Hamriya Nchini Sharja lenye ukubwa wa Square Kilo Mita 25 na wafanyakazi zaidi ya Laki moja hivi sasa lina Divisheni saba za viwanda mbali mbali ambapo tayari limeshasajili Makampuni yapatayo 62,000 hadi mwaka huu wa 2013 likiwa na uwekezaji unaokadiriwa kugharimu zaidi ya Dola za Kimarekani Bilioni kumi na Tano { U$ 15,000,000,000 }.

Wakati huo huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alikutana na Ujumbe wa Kampuni ya Kimataifa inayojishughulisha na Ujenzi wa Viwanja vya Ndege pamoja na Bandari { HELIOEST GROUP } ulioongozwa na Mwenyekiti wake Bwana Jean Marc Ciccotti.

Katika mazungumzo yao yaliyofanyika katika Hoteli ya Kitalii ya Pullman Dubai Balozi Seif aliuomba Uongozi wa Kampuni hiyo kungalia maeneo unaoweza kuwekeza katika ujenzi wa Bandari na uwanja wa ndege.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hivi sasa iko katika mipango ya kutaka kutanua Bandari yake ya Malindi Zanzibar pamoja na Uwanja wa ndege wa Pemba ili kuongeza harakati za kiuchumi.

Aliueleza ujumbe huo kwamba uwanja wa ndege Kisiwani Pemba unashindwa kutoa huduma za ndege kwa saa ishirini na nne kutokana na ukosefu wa Taa za kuongozea ndege wakati wa usiku.
“ Nadhami mkiamua kuharakisha kuleta maombi yenu Zanzibar tunaimani kwamba mtakuwa umeisaidia sana Serikali, Wananchi na hata wageni wanaoamua kutumia usafiri wa ndege nyakati za usiku kutoka au kuingia Pemba kwa usafiri wa anga “. Alisema Balozi Seif.

Sharja ni miongoni mwa Nchi saba zinazounda Muungano wa Falme za Kiarabu { UAE } ambazo ni Dubai, Abudhabi ikiwa Makao Makuu, Ras Al – Khaimah, Ajimani, Al –Fujaira pamoja na Umu Aquen.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top