Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itajitahidi kuona changamoto zinazowakabili watendaji wa Ofisi ya Uratibu wa shughuli za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar waliopo Dar es salaam zinashughulikiwa vyema kwa kupatiwa ufumbuzi ili kuleta ufanisi katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku. 

Kauli hiyo imetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alipofanya ziara maalum ya kuangalia shughuli za kazi za watendaji wa Taasisi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zilizopo Dar es salaam akianzia na Ofisi ya Uratibu wa shughuli za Serikali. 

Ofisi hiyo iliyopewa mamlaka ya kuratibu uwajibikaji wa Taasisi zote za SMZ zilizopo Mjini Dar es salaam itakuwa chini ya Ofisi Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kufuatia mabadiliko yaliyofanywa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr. Ali Mohammed Sheni katika baadhi ya Taasisi za Serikali siku moja iliyopita. 

Balozi Seif alisema Serikali iliamua kwa makusudi kuanzisha Ofisi hiyo mnamo mwaka 1986 kwa lengo la kuwa kiunganishi cha upatikanaji wa huduma za kiuchumi kiurahisi kati ya Zanzibar na Tanzania Bara sambamba na mashirika pamoja na Taasisi za Kimataifa. 

Katika mbinu za kujaribu kupunguza matumizi ya uendeshaji wa Ofisi Balozi Seif alifahamisha kwamba Serikali ina nia ya kulipata jengo hilo kwa kuwasiliana na Serikali ya Muungano hata kwa njia ya kubadilishana { Butter system } jambo ambalo gharama zinazotumika hivi sasa zinaweza kusaidia masuala mengine. 

Akizungumzia Kitengo cha Habari kilichojumuisha Magazeti ya Serika { Zanzibar Leo }, shirika la Utangazaji Zanzibar { ZBC } na Habari Maelezo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwapongeza wana Habari hao kwa umahiri wao wa kufanya kazi licha ya kuzunguukwa na mazingira magumu ya kikazi likiwemo tatizo la usafiri . 

Aliuagiza Uongozi wa Taasisi hizo kufanya utaratibu wa kuandika mapendekezo ya vile vifaa muhimu zaidi vya mwanzo na kuyawasilisha Serikalini ili kuangalia namna ya kusaidia uwezeshaji.

Balozi Seif alisema kutokana na mabadiliko ya haraka na ya kila wakati katika sekta ya Habari, watendaji wake wanalazimika nao muda wote waende na wakati. 

“ Kwa vile Serikali Kuu tumeshaamua Sekta zetu za Habari zijiendeshe kibiashara. Sasa Baraza letu la Wawakilishi kuanzia mwezi Oktoba katika vikao vijavyo litalazimika kulipa matangazo ya moja kwa moja ya vituo vya Habari vya ZBC Redio na Tv “. Alisisitiza Balozi Seif. 

Aliuagiza Uongozi wa Sekta ya Habari kufanya utafiti utakaofahamu tatizo linalosababisha matangazo ya ZBC Redio na Televisheni kutopatikana katika maeneo ya Tanzania Bara. 

“Mimi nilikuwa msikilizaji mkubwa wa Vipindi vya Redio hasa kile cha kutoka magazetini hakinipiti ninapokuwa Dar pamoja na matangazo ya ZBC TV. Hata nikiwa Dodoma Matangazo ya Redio nilikuwa nikiyapa lakini sasa yote yamekatika siju kwa nini? “ Aliuliza Balozi Seif. 

Mapema Mkurugenzi wa Shughuli za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Dar es salaam Shumbana Taufiq alisema Taasisi hiyo ambayo ni kiunganishi muhimu cha mawasiliano kati ya Zanzibar na Mashirika na Taasisi za Kimataifa imekuwa na mazingira magumu ya utekelezaji wa majukumu yake kutokana na tatizo la kutoingiziwa fedha kwa wakati. 

Mkurugenzi Shumbana alisema gharama za kupanda kwa maisha hasa katika Jiji la Dar es salaam kumewafanya watendaji hao kuishi katika maisha ya kubahatisha suala ambalo hupunguza ari na moyo wa uwajibikaji. 

“ Wakati mwengine sisi wasimamizi tunakuwa katika hali ya unyonge wakati hata zile fedha za pencheni kwa wafanyakazi wastaafu zinachelewakutufikia na matokeo yake kuleta malalamiko kwa wazee wetu hao waliopo hapa Dar “. Alifafanua Mkurugenzi Shumbana. 

Nao baadhi ya watendaji wa taasisi hizo wakiwemo viongozi wao wa Wizara na Idara wamezitaja baadhi ya changa moto zinazokwaza utekelezaji wao wa kazi ikiwa ni pamoja na ukosefu wa vifaa vya kazi, usafiri pamoja na kuomba kuongezewa posho ili kukidhi mahitaji. 

Awali Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alizitembelea Ofisi ya Idara ya Uratibu, Kitengo cha Utawala na Rasilmali Watu, uratibu wa misaada na Mipango pamoja na ile ya wana Habari.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top