Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Miundo mbinu na Mawasiliano inakusudia kuwatumia Wataalamu wake kufanya utafiti utakaosaidia kupata ufumbuzi wa kudumu katika eneo la Kijito upele ambalo huleta usumbufu kwa wapita njia hasa wakati wa mvua nyingi.

Kauli hiyo imetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alipofanya ziara fupi ya kuangalia eneo linalopitisha maji katika bonde la kijito Upele ambapo Mtoto Mmoja wa Darasa la Kwanza la Skuli ya Kijito Upele aliyejuilikana kwa jina la Naifat Abdulla Mrisho kuteleza na kutumbukia mtaroni mapema asubuhi na hatimae kufariki Dunia.

Balozi Seif alifahamisha kwamba eneo hilo limekuwa likileta usumbufu wa kujaa maji kusababisha matatizo ya kukatika kwa bara bara na hatiamae kuleta usumbufu kwa watumiao bara bara hiyo.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kupitia Uongozi wa Skuli ya Kijito Upela ameipa pole familia iliyopatwa na msiba huo wa Kijana wao na kuwataka kuwa na subira katika kipindi hichi kigumu cha maombolezo.

Mapema Mwalimu Mkuu wa Skuli ya Kijito Upele Bibi Saada Rajab Ali alimueleza Balozi Seif kwamba kupatikana kwa maiti ya Mwanafunzi Naifat Abdulla kunatokana na juhudi kubwa zilizochukuliwa na Kikosi cha Zima moto na Uokozi mara tu baada ya kuarifiwa.

Mwalimu Saada alisema Askari hao wa Zimamoto na Uokozi walilazimika kuzibua mtaro huo unaopitisha maji kutoka sehemu ya kaskazini kuelekea Kusini na kufanikiwa kumuokoa akiwa tayari ameshafariki Dunia.

Akionyesha huzuni zake kutokana na Mtihani huo Mwalim Saada ameishukuru Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kwa kuungana na Uongozi wa Skuli hiyo pamoja na Familia ya marehemu kwa kujitolea kugharamia mazishi yote ya Mwanafunzi Naifat Abdulla Mrisho.

Naye Mmoja wa Wazee wa Kamati ya Skuli ya Kijito Upele Bwana Manafi Said Mwinyi aliiomba Serikali kulifanyia marekebisho ya haraka eneo hilo ili kuondosha hali ya wasi wasi kwa wapitao eneo hilo.

Bwana Manafi alisema mabomba yaliyotumika kwenye kivuko hicho hivi sasa hayahimili tena kasi ya maji yanayopita sehemu hizo na kusababisha maji hayo kutapakaa katika bara bara na kuleta hofu hasa kwa watoto.

Marehemu Naifat Abdulla Mrisho anayekadiriwa kuwa na umri wa kati ya miaka saba na minane alikuwa akielekea Skuli yeye na wenzake na kupatwa na maafa hayo wakati wakijaribu kuipisha gari kwa kuhofia kurushiwa maji huku mvua zikiendelea kunyesha mapema asubuhi.

Othman Khamis Ame
 Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top