Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema  Mmiliki wa Kiwanja kilichopo maeneo ya pembezoni mwa Bwawa  la Mwanakwerekwe Bwana Mwalimu Mussa Khamis  anaweza kuendelea na ujenzi wa nyumba katika Kiwanja chake endapo atakubali kufuata masharti yote aliyoagizwa na Idara ya Mipango Miji.
Balozi Seif alitoa agizo hilo mara baada ya kufanya ziara ya ghafla katika eneo hilo lililokuwa likileta mgongano kati ya mmiliki huyo na Taasisi zinazosimamia Mipango Miji, Mazingira pamoja na  Baraza la Manispaa.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisema suala la kuzingatia Mipango Miji ni la msingi katika kuepuka maafa yanayoweza kuzuilika pamoja na kulinda mazingira.
Alisema mmiliki huyo alikuwa na uwezo wa kujenga nyumba yake ya kuishi kwa mujibu wa alivyopatiwa kiwanja hicho na Taasisi zilizohusika na ardhi lakini kilichojitokeza kwa mmiliki huyo kuchelewa  mno kuendelea na ujenzi huo.
“ ulikuwa na uwezo wa kujenga nyumba kwa mujibu wa mpango wa mwanzo lakini tatizo linalojichomoza ni kuchelewa mno ambapo yapo mabadiliko makubwa ya kimazingira katika eneo hili kwa hivi sasa”. Alisisitiza Balozi Seif.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alimshauri mmiliki wa kiwanja hicho kwamba kama tayari ameridhia masharti ya mamlaka ya mipango miji ataruhusiwa kuendelea na ujenzi wake.
Akitoa ufafanuzi wa tatizo hilo Kaimu Mkurugenzi wa Mipango Miji Bwana Abdulla Salum Rashid alisema taasisi yake ilizuia ujenzi huo baada ya mmiliki huyo kuamua kutaka kujenga jengo la Biashara la Ghorofa mbili.
Bwana Abdulla alisema pendekezo la mwanzo lililotolewa na Taasisi zinazosimamia masuala ya  ardhi lilimtaka mmiliki wa kiwanja hicho kujenga jengo la makaazi.
“ Kwa mujibu wa Mipango Miji ushauri uliotolewa jengo la eneo hilo liwe la Makaazi kama pendekezo la mwanzo lilivyoelekeza na sio jengo la Biashara tena la ghorofa mbili”. Alisisitiza Bwana Abdulla.
Mapema Mmiliki wa Kiwanja hicho Bwana Mwalimu Mussa Khamis alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif kwamba alipatiwa kiwanja hicho kwa mujibu wa taratibu za ugawaji wa Viwanja kutoka Taasisi za ardhi tokea mwaka 1999.
Bwana Mwalimu alisema amekuwa akipata vikwazo vya ujenzi huo na kupelekea Mhandisi wake kushindwa kuendelea na ujenzi kutokana na kukosa kibali cha ujenzi wakati taratibu zote tayari zilikuwa zimeshakamilika.
Eneo hilo la Kiwanja cha Bwana Mwalimu Mussa Khamis kiliopo kandoni mwa Bara bara iendayo Fuoni nyuma ya Bwana la Mwanakwerekwe kimepata athari ya kimazingira kutokana na kuchimbwa ovyo kwa mchanga katika miaka ya nyuma.
Othman Khamis Ame
Ofisi ya Mkamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top