Jamii imekumbushwa kuwa na tahadhari kufuatia mvua kubwa zinazoendelea kunyesha nchini ambazo tayari zimeshaleta athari na kupoteza maisha ya watu kadhaa katika baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Dar es salaam.
Tahadhari hiyo imetolewa na Wajumbe wa Kamati ya Taifa ya kukabiliana na Maafa Zanzibar Chini ya Mwenyekiti wake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi kujadili maafa yaliyowakumba Wananchi hao wa Dar es salaam pamoja na kuchukua jitihada za kujikinga na maafa endapo yatatokea hapa Zanzibar.
Wajumbe hao walisema mafuriko mara nyingi huwakumba watu wanaoishi katika sehemu za mabonde. Hivyo ni vyema wakawa makini katika kipindi hichi cha mabadiliko ya hali ya hewa.
“ Tumejifunza matukio ya majanga yanapotokezea hasa mafuriko na ajali za bara barani na baharini, sasa tunahitajika kuwa makini katika kukabiliana na athari kama hizo wakati zinapotokea ”. Alisisitiza Kamishna wa Polisi Zanzibar Mussa Ali Mussa.
Wajumbe hao wameziagiza Taasisi zote Nchini kuhakikisha kwamba zinawajibika vyema katika maeneo yao kwa lengo la kuwa tayari kwa athari yoyote inayoweza kutokea.
Pamoja na mambo mengine Kikao hicho kimeamua kupeleka ujumbe wa watendaji na Wataalamu wa Vikosi vya SMZ kufuatilia athari zilizotokea huko Dara es salaam na kuona namna ya kusaidia.
Ujumbe huo utakaoshirikisha pia Wakuu wa Vikosi vya SMZ utaongozwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar Mh. Mohd Aboud Mohd.
Akikiahirisha Kikao hicho cha Wajumbe wa Kamati ya Taifa ya kukabiliana na Maafa Zanzibar Mwenyekiti wa Kamati hiyo Balozi Seif Ali Iddi alisema Serikali itaendelea kutoa hadhari kadri hali ya matokeo yanavyojitokeza.
Kufuatia mabadiliko hayo ya hali ya hewa Wananchi wameombwa kuchemsha maji ili kujikinga na maradhi ya mripuko pamoja na kuchukuwa tahadhari kwa wale wanaoishi katika sehemu za mabonde.
Mvua hiyo kubwa kuwahi kutokea katika historia ya Tanzania Bara tokea mwaka 1956 imesababisha vifo vya watu kadhaa, kuvunjika kwa madaraja, bara bara na maelfu ya watu kutokuwa mahali pa kuishi kutokana na nyumba zao kujaa maji

0 comments:

 
Top