Uongozi wa Idara Maalum ya Chuo cha Mafunzo Zanzibar umeshauriwa kuandaa utaatibu maalum wa kutoa mafunzo ya Kilimo kwa Vijana kwa lengo la kuwasaidia kupata ajira ya kudumu ya kuendesha Maisha yao.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ametoa ushauri huo wakati wa ziara yake ya kutembelea Idara Maalum ya Chuo cha Mafunzo hapa unguja ili kujifunza na kuelewa matatizo yanayokikabili Kikosi hicho.
Balozi Seif alisema licha ya kikosi hicho kutoa taaluma kwa Wanafunzi wenye makosa mbali mbali ili wawe raia wema wa baadaye lakini bado Taasisi hiyo kwa ujuzi iliyonao bado ina nafasi ya kuwasaidia vijana ili kuipunguzia mzigo wa ajira Serikali Kuu.
Alisema Vijana wengi wanahitaji maeneo ya uzalishaji pamoja na kupatiwa ushauri na Taaluma ili waondokane ile tabia ya kukaa mitaani kwa mawazo ya kusubiri ajira ya Serikali.
“ Ni vyema Jeshi likatafakari kuangalia njia za kuwasaidia Vijana ambao wengi wanaendeleza tabia ya kukaa Vijiweni. Na hii itakuwa dawa ya kuwasaidia kujiepusha na vitendo viovu ”. Alisema Balozi Seif.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alikipongeza Kikosi hicho kwa jitihada zake za kuimarisha Sekta ya Kilimo ambayo ndiyo uti wa mgongo wa Taifa hili.
“ Nimevutiwa na Juhudi zinazochukuliwa na Kikosi hichi katika uzalishaji katika sekta ya Kilimo ambao unaongeza chakula”. Alisisiiza Balozi seif.
Akizungumzia suala la migogoro ya ardhi inayojitokeza baina ya baadhi ya Makambi ya Kikosi hicho na Wananchi walio jirani Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisema ardhi ni mali ya Serikali.
Hinvyo alisema serikali ina wajibu wa kulitumia eneo lolote la ardhi pindi inapoonelea kufanya hivyo kwa matumizi ya Taasisi zake au hata huduma za kijamii ambazo huwagusa moja kwa moja Wananchi.
Balozi Seif alikumbusha kwamba kinachojitokeza wakati wa matumizi hayo ya Ardhi ni ulipwaji wa fidia kwa vipando na Majengo ya Wananchi yaliyomo katika meneo hayo.
Hivyo alieleza kwamba Wananchi wana wajibu wa kulielewa hilo vyenginevyo wakianza kupiga kelele watakuwa hawaitendei haki Seriikali yao.
Katika Taarifa zao kwenye mbali Vyuo mbali alivyovitembelea Balozi Seif wapiganaji hao wa Idara Maalum ya Chuo cha mafunzo wameelezea matatizo kadhaa wanayo kabiliana nayo ikiwa ni pamoja na Ukosefu wa Matrekta ya Kulimia mazao mbali mbali na Uchakavu wa baadhi ya Majengo yao.
Wapiganaji hao wamesema Vyuo vingi vimekuwa vikitegemea zaidi sekta ya kilimo kwa uzalishaji ili kupata vyakula kwa ajili ya wanafunzi pamoja na kuongeza pato la Idara hiyo.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alianzia ziara yake ya Idaya ya chuo cha mafunzo kwa kukagua shughuli zao za kila siku hapo Makao Makuu yao Kilimani.
Baadaye Balozi Seif aliangalia shughuli za Kilimo cha Muhogo na Mpunga katika shamba la chuo cha mafunzo cha Kinu Moshi, shamba la kilimo Langoni, ujenzi wa Nyumba za Wanafunzi Ubago, pamoja na kukagua eneo la ekari 40 linalotazamiwa kujengwa Jengo la Kisasa la Wanafunzi huko Hanyegwa Mchana.
Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top