Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balizi Seif Ali Iddi amewaasa Wazee Nchini kuwadhibiti watoto wao kutojiingiza katika makundi yanayoandaliwa na baadhi ya watu wakiwemo wanasiasa kufanya vurugu zinazoashirika kutaka kuvuruga amani ya Nchi.

Akaonya kwamba asijetokea mzazi atakayetaka kuilaumu Serikali wakati vyombo vyake vya dola vitakavyotekeleza majukumu yake katika kuwadhibiti watu watakaobainika kusababisha vurugu ndani ya kipindi hichi kinachoelekea kwenye uchaguzi Mkuu wa Mwezi Oktoba.

Balozi Seif Ali Iddi ambae pia ni Mbunge wa Jimbo la Kitope alitoa wosia huo wakati akikabidhi mchango wa shilingi Milioni 4,000,000/- akitekeleza ahadi aliyotoa tarehe 4 June mwaka huu kusaidia matengenezo ya uwanja wa michezo wa Timu ya soka ya Fujoni Boys { HIBURY } hafla iliyofanyika katika Maskani ya Nia Njema Nyumba ya Ndege Fujoni.

Balozi Seif alisema Serikali ina taarifa kwamba wapo watu na baadhi ya wanasiasa waliojiandaa kifedha kuwashawishi vijana kujiingiza katika makundi na kufanya vurugu ndani ya zoezi la uandikishaji wa vitambulisho vya kupiga kura pamoja na uchaguzi wa mwezi Oktoba.

Aliwatahadharisha Wazazi pamoja na Vijana kwamba Serikali kupitia vyombo vyake vya Dola iko makini na tayari imeshajiandaa kukabiliana na vurugu ama njama yoyote itakayoandaliwa ya kutaka kujaribu kutia doa zoezi hilo la uandikishaji wapiga kura pamoja na uchaguzi Mkuu.

Alifahamisha kwamba inasikitisha kuona mtego huo unaoandaliwa na kuwahusisha zaidi Vijana mara zote unafanywa na watu wanaokuwa mbali na matatizo yanayowakumba vijana hao baada ya kuhusika na vurugu hizo.

“ Wazee lazima wajizatiti katika kuhakikisha wanawanusuru watoto wao na mtego unaoandaliwa na watu wenye nia na muelekeo wa maslahi yao binafsi “. Alisema Balozi Seif.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alieleza kwamba wapo Watu na baadhi ya makundi yasiyoitakia kheir nchi hii ambao tayari wameshaanza kuonyesha dalili za kuleta Vurugu.

Balozi Seif aliwahakikishia Wananchi wote Nchini kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Ile ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania zitajitahidi kuona amani na utulivu wa Nchi unaendelea kudumu katika muda wote.

Akigusia kitendo cha Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wa Chama cha Wananchi { CUF } kutoka kwenye Kikao cha Baraza la Wawakilishi kilichokuwa kikiendelea kwenye Baraza hilo Mbweni hapo juzi Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisema uamuzi wao haukuzingatia upeo wa Demokrasia ya mfumo wa vyama vingi wa Siasa uliopo hapa Nchini.

Balozi Seif akiwa Mtendaji Mkuu wa Serikali alielezea masikitiko yake kutokana na uwamuzi wa Wajumbe hao wa Upande wa Upinzani uliokuwa na nia ya kutaka kuvuruga mfumo mzima wa muenendo wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar unaofuata Mfumo wa Umoja wa Kitaifa.

Alisema ususiaji wa Wajumbe hao katika Vikao vya Baraza hilo lililokuwa likijadili na kutaka kupitisha matumizi ya Serikali yalikuwa na lengo la kutaka kuzuia matumizi halisi ya fedha kwa Taasisi za Umma za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar jambo ambalo lingevuruga mfumo mzima wa uendeshaji wa Serikali.

“ Licha ya misaada ya baadhi ya wahisani lakini fedha nyingi zinazotumika kwenye uchaguzi wetu zinatoka katika mfuko Mkuu wa Serikali. Sasa mbinu za Wajumbe hao kukimbia kupitisha makadirio ya matumizi kwa Wizara inayosimamia fedha zinaashiria kutaka kuharibika kwa uchaguzi Mkuu “. Alifafanua Balozi Seif.

Mapema Mke wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mama Asha Suleiman Iddi alisema Viongozi na wanachama wa vyama vya Upinzani ni vyema wakazingatia umuhimu wa kuwa na uvumilivu wa kisiasa ndani ya mfumo wa vyama vingi vya siasa hapa Nchini.

Mama Asha alisema yapo mambo na baadhi ya matukio yenye kuleta kero na hata usumbufu kwa Viongozi na Wanachama wa Chama cha Tawala cha CCM lakini wana CCM hao wanalazimika kukubali kuvumilia kwa lengo la kudumisha amani na upendo miongoni mwa jamii.

Amewapongeza Wananchi wa Fujoni kwa msimamo wao madhubuti wa kulinda na kutetea sera za Chama Tawala cha Mapinduzi zilizopata ridhaa za wananchi walio wengi kwenye uchaguzi wa mwaka 2010 na kupata fursa ya kuongoza Dola.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top