Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema kwamba Ushirikiano wa karibu unaozijumuisha Nchi za Jumuiya ya Mataifa ya Ukanda wa Kusini mwa Bara la Afrika SADC katika masuala ya Ulinzi wa Anga umesaidia kudhibiti changamoto za Amani na Usalama ndani ya ukanda huo.

Alisema uanzishwaji wa Kituo cha pamoja cha uchunguzi wa usalama wa Anga { Exercise Blue Okavango } katika Mataifa wanachama wa Jumuiya hiyo ya SADC umeleta mafanikio makubwa.

Balozi Seif Ali Iddi alieleza hayo wakati akiufunga Mkutano wa 17 wa siku mbili wa Wakuu wa Majeshi ya Anga wa Nchi za Kusini mwa Bara la Afrika { SADC – SAC } uliokuwa ukifanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Zanzibar Beach Resort Mzizini nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.

Alisema ndoto iliyobuniwa na Viongozi wa Mtaifa wanachama katika kuanzisha taasisi hiyo ya ulinzi wa pamoja wa Anga imelenga kuwajengea mazingira bora ya ustawi wa kuishi kwa amani na utulivu Wananchi wote wa ukanda wa Sadc.

“ Tunapaswa kuangalia kwa umakini hatma ya harakati za utendaji wa Taasisi yetu tuliyoipa jukumu la ulinzi wa Anga katika hali ya uaminifu kwa hatma njema ya baadaye “. Alisema Balozi Seif.

Balozi Seif alielezea faraja yake kutokana na Uongozi wa Kamati Kuu ya Wakuu wa Majeshi ya Anga wa Nchi za Kusini mwa Bara la Afrika { SADC – SAC } kufanya kazi kwa pamoja.

“ Mafanikio ya uendeshaji wa Kituo cha pamoja cha uchunguzi wa usalama wa Anga { Exercise Blue Okavango } cha Jumuiya hiyo yametokana na mchango mkubwa unaotolewa na Kamati hiyo “. Alifafanua Balozi Seif.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliupongeza Uongozi wa Kikosi cha Anga cha Jeshi la Wananchi wa Tanzania kinachoongozwa na Kamanda Mkuu wa Kikosi hicho Meja Jenerali Joseph Furaha Kapwani kwa kufanikisha vyema Mkutano huo wa 17 wa SADC – SAC hapa Zanzibar.

Balozi Seif aliwaomba Makamanda washiriki wa Mkutano huo kutoka nchi wanachama wa Jumuiya hiyo kuwa Mabalozi wazuri wa kuitangaza Zanzibar katika Mataifa yao kwa mazingira mazuri waliyoyaona ya uwekezaji ambayo wale watakaopata fursa wanaweza kuitumia nafasi hiyo.

Akitoa shukrani kwa niaba ya washiriki wa Mkutano huo wa 17 wa Sadc – Sac Mkuu wa Majeshi ya Anga wa Jamuhuri ya Botswana Meja Jenerali Mashinyana amewashukuru na kuwapongeza Wazanzibar na Watanzania kwa ujumla kutokana na ukarimu waliouonyesha.

Kamanda Mashinyana alisema utulivu walioupata yeye pamoja na Makamanda wenzake wa Mataifa wanachama wa Sadc – Sac wakati wakiwa Zanzibar umewapa faraja kubwa watayoendelea kuikumbuka katika maisha yao hata wakati wameshastaafu kazi ya ulinzi.

Washiriki wa Mkutano huo wa 17 wa siku mbili wa Wakuu wa Majeshi ya Anga wa Nchi za Kusini mwa Bara la Afrika { SADC – SAC } pia walipata fursa ya kutembelea sehemu mbali mbali za Kihistoria pamoja na maeneo ya matunda na Viungo.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top