Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema yapo matumaini makubwa ya kukua kwa Uchumi wa Zanzibar kukua ambako kutategemea pia Uchaguzi Mkuu wa Mwezi wa Oktoba mwaka huu kama utakwenda kwa amani na utulivu.

Alisema Serikali kwa upande wake itahakikisha Tume ya Uchaguzi Zanzibar inaendesha Uchaguzi wenye uwazi, huru na haki kwa wagombea wote watakaobahatika kushiriki kwenye uchaguzi huo.

Balozi Seif Ali Iddi akiwa kiongozi wa shughuli za Serikali alisema hayo wakati akiifunga Semina ya siku Nne ya Wajumbe wa Bawaza la Wawakilishi pamoja na watendaji Wakuu wa Serikali juu ya uchambuzi wa Bajeti na Masuala ya Uchumi iliyokuwa ikifanyika katika ukumbi wa Z Ocean Hoteli Chuwini Wilaya ya Magharibi “A”.

Alisema Uchaguzi ulio salama na haki utakuwa kichocheo kikubwa kitakachotoa fursa ya kusaidia kukua kwa uchumi wa Taifa sambamba na kuhamasiha wawekezaji wengi zaidi kumiminika nchini kwa lengo la kuwekeza miradi yao ya Kiuchumi.

Balozi Seif aliwanasihi wanasiasa ni vyema wakajiepusha na kauli za kuchochea vurugu, huku akiwataka wananchi kutokubali kuchochewa kuanzisha fujo wakati Waandishi wa Habari wakawajibika ipasavyo kutekeleza majukumu yao kwa jamii katika misingi ya uadilifu.

“Sifikiri kabisa kwamba kutakuwepo au kuja kwa muwekezaji kutaka kuanzisha miradi ya kiuchumi wakati atashuhudia pamoja na kuona utulivu wa amani unakosekana kutokana na fitna na baadhi ya watu “. Alisema Balozi Seif.

Akizungumzia umuhimu wa kutunza Mazingira Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alitahadharisha kwamba Jamii ikiendelea kuchafua mazingira ielewe kwamba Mvua zitapungua na hatimae kuathiri Sekta ya kilimo kwa kiasi kikubwa.

Alifahamisha kwamba utunzaji wa mazingira kwa kila Taasisi au Mtu ni jambo la lazima kutokana na Wananchi walio wengi Zanzibar wanbategemea Kilimo katika kuendesha maisha yao.

Balozi Seif alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana na Taasisi tofauti wakiwemo washirika wa Maendeleo itaendelea kudhibiti uchafuzi wa mazingira kwa kasi zaidi ikiwemo kutunza vianzio vya Maji.

Kuhusu Bajeti inayozingatia matokeo { PBB } ambao ni mfumo mpya utakaotumika katika majadiliano ya Baraza la Wawakilishi kwenye Bajeti ya mwaka huu Balozi Seif alisema mfumo huu utawasaidia Wananchi kuelewa kwa uwazi Bajeti ya Serikali yao na imeleta matokeo gani kwao.

Alisema Mfumo huu mpya ambao utawapa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kuendelea kujifunza unasaidia kujenga uwazi katika suala zima la matumizi ya Serikali jambo ambalo ni muhimu katika jitihada za kukuza uchumi wa Wananchi.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliotoa wito kwa Wizara ya Fedha kuendeleza jitihada zake za kuelimisha watendaji wa Taasisi za Serikali ili Mpango wa Bajeti inayozingatia matokeo { PBB } ufahamike vizuri zaidi.

“Mpango wa Bajeti inayozingatia matokeo { PBB } itatusaidia kuelewa walengwa wa program ni nani, program itatoa huduma gani “. Alifafanua Mtendaji Mkuu huyo wa Shughuli za Serikali.

Mapema Mshauri wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar Bwana Mussa alisema mfumo mpya wa Bajeti { Bajet Office } tayari umeshaanzishwa na Mabunge mengi Ulimwenguni yakiwemo pia baadhi ya Mabunge ya Afrika.

Bwana Mussa alisema Baraza la Wawakilishi Zanzibar limeanza na maandalizi ya kutumia mfumo huu mpya tokea mwaka 2012 kwa hatua za awali ambao utekelezaji wake unaweka wazi matumizi ya Serikali.

Akiwasilisha majumuisho ya wanasemina Ndugu Hamad alisema Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi pamoja na watendaji wakuu wa Serikali walipendekeza uwepo wa ubunifu katika uimarishaji wa vianzio vya mapato ya ndani.

Nd. Hamadi alisema mageuzi Katika uwajibikaji lazima uanzie kwa viongozi na baadaye kuteremka kwa wananchi sambamba na changamoto mbali mbali zinazokwaza utekelezaji wa Mpango wa Kupunguza Umaskini Zanzibar { MKUZA } ziondolewe.

Aidha alieleza kuwa washiriki wa Semina hiyo wakapendekeza pia kuwepo kwa Bajeti inayozingatia jinsia ijielekeze katika kutatua changamoto za Wanawake, Watoto pamoja na Makundi Mengine.

Semina hiyo ya siku Nne ya kujifunza Mpango wa Bajeti inayozingatia matokeo { PBB } pamoja na mambo mengine imejadili mada mbali mbali zikiwemo hali ya Uchumi, Idadi ya watu na Maendeleo, Uwazi na Uwajibikaji pamoja na Wajibu wa Baraza la Wawakilishi wa kusimamia Bajeti.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top