Na: Hassan Hamad, OMKR.
Wazee wa Chama Cha Wananchi CUF kisiwani Pemba wameuomba uongozi wa Chama hicho kuandaa utaratibu bora wa kutoa elimu ya wapiga kura, ili kuhakikisha kuwa wanachama wote walioandikishwa wanashiriki katika zoezi la upigaji kura katika uchaguzi mkuu ujao.

Wakichangia mjadala kuhusu maandalizi ya uchaguzi mkuu mbele ya Katibu Mkuu wa Chama hicho Maalim Seif Sharif Hamad, kwenye kikao maalum cha wazee wa CUF kilichofanyika Ofisi za CUF Mkanjuni Chake Chake Pemba, wazee hao kutoka Wilaya nne za Pemba wamesema ni aibu kwa baadhi ya wanachama kutoshiriki upigaji kura, jambo ambalo linachangia kukikosesha ushindi chama hicho.

Kauli hiyo imekuja baada ya kuwepo taarifa kuwa wananchi kadhaa kisiwani Pemba hawakushiriki upigaji kura katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.

Akichangia mjadala huo, mzee Mohammed Ali Salim kutoka Wilaya ya Mkoani amesema elimu zaidi ya wapiga kura inahitajika, ili kuhakikisha kuwa kila aliyeandikishwa kuwa mpiga kura anaitumia fursa hiyo.

Wazee hao pia wameelezea haja ya kupatikana kwa vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi (ZAN ID) kwa wakati muafaka, ili walionavyo waweze kuandikishwa katika daftari la kudumu la wapiga kura mwezi ujao.

Wamesema baadhi ya wananchi Kisiwani Pemba tayari wameshajiandikisha na kupewa risiti, lakini bado hawajapatiwa vitambulisho vyao kwa takriban mwaka mmoja sasa. Hivyo wameiomba taasisi inayohusika kurahisisha zoezi hilo.

Akijibu hoja hizo, Mkurugenzi wa Mipango na Chaguzi wa CUF Mhe. Omar Ali Shehe amesema Chama hicho kimejiandaa kutoa elimu kwa wapiga kura ili kuhakikisha kuwa kasoro zilizojitokeza katika uchaguzi wa mwaka 2010 hazitokei tena.

Kuhusu vitambulisho, Mkurugenzi huyo amesema licha ya kuchelewa kwa vitambulisho hivyo, lakini baadhi ya watu wameshindwa kuchukuliwa vitambulisho vyao vya kupigia kura katika ofisi za tume ya uchaguzi, na kuwahimiza kwenda kuvichukua.

Mapema akiwahutubia wazee hao, Katibu Mkuu wa CUF Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, amesema tayari Chama hicho kimeshapata uzoefu wa kutosha wa masuala ya kisiasa, na kuwataka wazee hao kujiandaa kwa ajili ya ushindi katika uchaguzi ujao.

Aidha amewataka kushirikiana na vijana ili kulinda na kudhibiti mianya inayopelekea kupotea kwa kura za Urais, tofauti na kura za Ubunge na Uwakilishi.

0 comments:

 
Top