Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Mizengo Peter Pinda aliwapongeza wanamichezo wa Timu za Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuliletea sifa kubwa Bunge hilo kwenye mashindano ya michezo mbali mbali ya Kitaifa na Kimataifa.

Mh. Pinda alitoa pongezi hizo katika Tafrija maalum ya kuukaribisha mwaka mpya zilizofanyika katika majengo ya Bunge la Jamuhuri Mjini Dodoma hafla iliyokwenda sambamba na kuwapongeza wanamichezo wa Bunge hilo baada ya kushinda michezo tofauti katika mashindano ya Mabunge ya Jumuiya ya Afrika Mashariki yaliyofanyika Mjini Arusha Tanzania.

Waziri Mkuu Pinda alisema kwamba michezo inatoa nafasi kubwa ya ushirikiano ambayo ni kielelezo cha msingi kinachozaa Viongozi bora wanaotokana na sekta ya michezo.

Aliishauri Kamati ya Uongozi wa Michezo ya Bunge hilo kufikiria umuhimu wa kuwashirikisha wawakilishi wa wanamichezo wa mabunge wanachama kwenye tafrija kama hizo kwa lengo la kusherehekea nao pamoja ili kudumisha ushirikiano pamoja na ujirani mwema.

Alieleza kwamba michezo ina nafasi pana ya kupunguza joto la kisiasa, hitilafu au ugomvi unaotokea baina ya nchi na nchi na kupelekea watu wa pande zinazohitilafiana kurejea kwenye ushirikiano na mafungamano baina yao.

Mh. Pinda alifahamisha kwamba kwa kuwa mabunge mengi yana utaratibu mzuri wa kuandaa mashindano ni vyema kwa waheshimiwa wabunge kuzitumia fursa kama hizo katika kushiriki kwenye mazoezi na hatimae mashindano kwa lengo la kudumisha afya zao.

Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania aliwatakia mwaka mwema wa 2015 Waheshimiwa wote wa Bunge la Jamuhuri hasa mwezi Oktoba mwaka huu ambao kama wamefanya vyema majimboni mwao utawarejesha tena kwenye wadhifa wao.

Alisema kurejea kwa Wabunge hao kwa kiasi kikubwa kunaweza kuleta faraja kubwa kwa vile tayari wameshazoeana kutokana na kushirikiana pamoja katika vikao vya Bunge hilo kwa takriban miaka mitano.

Mapema Mwenyekiti wa Bunge Sports Club Iddi Azan alisema ongezeko la michezo mbali mbali kwenye mashindano ya Timu za Mabunge ya Afrika ya Mashariki linatokana na azimio la Mabunge ya Jumuiya hiyo la kuzitaka Nchi Wanachama kuongeza michezo mengine kwenye mashindano hayo.

Mwenyekiti Azan alisema mshindano ya Mabunge hayo yalikuwa yakishirikisha michezo miwili tuu ile ya Kandanda na Pete ambapo kwa sasa ipo riadha, mbio za vijiti, kuvuta kamba, kufukuza kuku ikiwemo pia ile ya watu wenye mahitaji maalum { Walemavu }.

Mwenyekiti huyo wa Bunge Sports Club alielezea faraja yake kutokana na ushiriki mzuri wa wanamichezo wa Timu za Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye mashindano mbali mbali ya Mabunge na kuleta ushindi katika michezo tofauti.

Katika mashindano hayo ya mwaka 2014 ya Timu za Mabunge ya Jumuiya ya Afrika Mashariki yaliyoshirikisha wachezaji 150 Timu ya Mpira wa Pete Wanawake ya Bunge la Tanzania ilitokea mshindi wa kwanza, Riadha wanawake washindi wa kwanza, riadha wanaume washindi wa Tatu, mpira wa miguu washindi wa Pili na kuvuta kamba Timu za wanawake na wanaume Tanzania zimeshika nafasi ya kwanza.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top