Na Bashir Nkoromo

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinaingia katika uchaguzi wa serikali za mitaa kesho, kikiwa kimeshajizolea maelfu ya nafasi ambazo wagombea wake wamepita bila kupingwa.

Akihutubia kwenye mkutano wa kufunga kampeni za uchaguzi huo, 
katika Mtaa wa Mtambani B, Kata ya Jangwani, jimbo la Ilala jijini Dar es Salaam, Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi Nape Nnauye alisema, kulingana na takwimu CCM imepita bila kupingwa katika vijiji 2708, mitaa 644, na vitongoji zaidi ya 26,300.

Alisema, CCM imeweza kupita bila kupigwa baada ya vyama vya upinzani kushindwa kusimamisha kabisa wagombea na maeneo mengine kuweka wagombea ambao walionekana kukosa sifa za kugombea baada ya kuwekewa pingamizi.

Nape alisema, hatua hiyo ya CCM kuingia kwenye uchaguzi huo ikiwa na mtaji mkubwa wa nafasi ambazo wagombea wake amepita bila kupingwa ni dalili tosha kwamba chama kitavibwaga vibaya vyama vya upinzani kuliko uchaguzi uliopita mwaka 2009.

"Uchaguzi uliopita wa serikali za mitaa CCM iliibuka na ushindi wa asilimia 96, sasa kutokana na dalili za mapema, uchaguzi wa safari hii sina shaka kabisa kwamba wapinzani tutawapiga kwa ushindi wa asilimia mia moja", alisema Nape.

Nape aliupongeza uongozi wa CCM katika jimbo la Ilala, baada ya kumthibitibishia kwamba katika kipindi chote cha kampeni jimbo hilo 
wamekuwa wakifanya kampeni za kistaarabu na wanao uhakika wa 
kuibuka na ushindi kwa asilimia mia moja baada ya uchaguzi.

"Sina shaka kabisa kwamba hapa Ilala tutashinda kwa kishindo, mnastahili kupata pongezi kutoka makao makuu kutokana na mlivyoendesha kampeni, hongereni sana.". alisema Nape.

Alisema, pamoja na CCM kuwa na uhakika wa kushinda lakini itafanya kazi ya ziada ya kuhakikisha wapigakura waliojiandikisha wanapata fursa ya kwenda kupiga kura bila kubughudhiwa na watu ambao huandaliwa na vyama vya upinzani kufanya fujo ili kuzuia watu wasijitokeze kupiga kura.

"Nasema bila kificho, vijana wa CCM kama mtamuona mtu yeyote anajaribu kufanya fujo wakati wa upigaji kura mshughulikieni kidogo kabla ya kumpeleka polisi, maana watu wa aina hii wanabaka demokrasia, lazima waadabishwe". alisema Nape na kuongeza.

"Vijana wa CCM lazima tuwe shupavu, maana kujifanya wanyonge unyonge huu hautatusaidia chochote, na hili mimi sihamasishi fujo na si wa kwanza kulisema hata Mwenyekiti wetu wa CCM alishasema kwamba unyonge basi. Sasa mimi hapa napigilia msumari tu".

Nape aliwataka wananchi wa Ilala na Watanzania kwa jumla kuchagua wagombea wa CCM, kwa kuwa ana uhakika ndio watakao watumikia vizuri.

Aliwataka viongozi watakaochaguliwa katika uchaguzi huo wa serikali za mitaa kuhakikisha wanawatumikia wananchi, hasa kwa kusimamia kuondoa kero zao na kusimamia misingi ya kuboresha mazingira ya shughuli mbalimbali zikiwemo za biashara kama za mamalishe na machinga.

Nape alisema, CCM, itaendelea kusimamia na kutetea haki za wananchi hasa walio wanyonge na si kwa sababu ya kutaka kura ila kwa sababu ni wajibu wake kama chama kilichopewa ridhaa ya kutawala nchi.

Katika mkutano huo, Nape aliwanadi wagombea wa nafasi mbalimbali katika Mtaa huo wa Mtambani B, akiwemo mgombea wa nafsi ya Ueneyekiti wa mtaa huo, Gungu Tambaza.

0 comments:

 
Top