Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, ameelezea kuridhishwa kwake na hatua iliyofikiwa katika ujenzi wa miradi mitatu inayoendelea kwenye uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume.

Miradi hiyo inahusisha ukarabati na ujenzi wa njia za kupitia ndege wakati wa kuruka pamoja na sehemu ya maegesho ya ndege, ujenzi wa uzio wa eneo la uwanja wa ndege, pamoja na ujenzi wa jingo jipya la abiria (Terminal 2).

Akizungumza katika ziara ya kutembelea miradi hiyo huko uwanja wa ndege wa Zanzibar, Maalim Seif amesema hatua iliyofikiwa inatia moyo, na kuwataka wakandarasi na wasimamizi wa miradi hiyo kuhakikisha kuwa inakamilika kwa wakati.

Amesema Serikali kwa upande wake itaweka mkakati wa makusudi ili iweze kumaliza kuwalipa fidia wananchi ambao bado hawajalipwa, na kuruhusu ujenzi wa uzio uweze kukamilika kwa akati.

Mapema meneja wa mradi wa ujenzi wa uzio huo Bw. Frederick Nkya, alimueleza Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar kwamba hadi sasa tayari asilimia 73 ya ujenzi huo imeshakamilika.

Hata hivyo amesema changamoto kubwa inayowakabili ni eneo la mita elfu tatu na mia moja ambapo sehemu kubwa ya eneo hilo bado wananchi hawajalipwa fidia.

Amefahamisha kuwa hadi sasa eneo la mita elfu mbili na mia saba ndilo ambalo halijafanyiwa tathmini kuweza kuwalipa wananchi walioko katika maeneo ya mradi huo.

Miradi ya ukarabati na ujenzi wa njia za kupitia ndege wakati wa kuruka (Taxiway) pamoja na sehemu ya maegesho ya ndege (Apron) katika uwanja huo inafadhiliwa na Benki ya Dunia pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ambapo mradi wa ujenzi wa uzio wenye urefu wa mita 11,690 katika uwanja huo, unatekelezwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pekee, ambapo zaidi ya shilingi bilioni sita zitatumika hadi kukamilika kwa mradi huo.

Kuhusu mradi wa ujenzi wa jengo jipya la abiria ambao awali ulikumbwa na changamoto mbali mbali ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa eneo la mradi, meneja wa mradi huo Bw. Ibrahim Zhang, amesema kazi hiyo sasa inaendelea vizuri.

Mradi wa ujenzi wa jingo jipya la abiria awali ulitiwa saini mwezi wa Septemba 2009 baina ya Wizara ya Miundo mbinu na Mawasiliano na Kampuni ya ujenzi ya Beijing Construction Engineering Group ya China, lakini baadae serikali iligundua kuwa ukubwa wa jengo uliopendekezwa mwanzo haukidhi haja.

Hivyo Serikali ilikubaliana na mkandarasi kuongezwa ukubwa wa jengo kutoka mita 15,600 hadi mita 17,800 kwa ongezeko la fedha dola za kimarekani milioni 11 nukta 8, na kufanya gharama za mradi huo kufikia dola la kimarekani milioni 82 nukta 2.

0 comments:

 
Top