Zaidi ya asilimia 95% imefikiwa katika ujenzi wa Matawi ya Kisasa ya Chama cha Mapinduzi ndani ya Jimbo la Kitope liliomo katika Wilaya ya Kaskazini “B” Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Hali hiyo imekuja kufuatia hatua za ukamilishaji wa Linta katika Tawi la Chama cha Mapinduzi la Kazole likiwa miongoni mwa Matawi 19 ya Kisasa yaliyo kwishajengwa kati ya Matawi 20 yaliyomo ndani ya Jimbo hilo.

Katika kuunga mkono harakati za Wanachama wa chama cha Mapinduzi wa Tawi la Kazole za ukamilishaji wa ujenzi wa Tawi lao Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM Balozi Seif Ali Iddi alikabidhi vifaa mbali mbali kwa ajili ya ukamilishaji wa linta na baadaye kujiandaa kwa uwezekaji.

Balozi Seif ambae pia ni Mbunge wa Jimbo la Kitope na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwaomba wanachama hao wa Tawi la CCM Kazole wajitahidi kukamilisha kazi hiyo ili wao pamoja na Uongozi wa Jimbo hilo ujizatiti katika hatua ya uwezekaji.

“ Ukweli nimefarajika sana kuona kwamba ile kiu yangu ya muda mrefu ya kuona Matawi yetu 20 yaliyomo ndani ya jimbo letu yanakamilika kujengwa katika mfumo wa kisasa kabla ya mwaka 2015 “. Alifafanua Balozi Seif.

Alisema Chama cha Mapinduzi wakati wote kimekuwa kikisisitiza wanachama wake Nchini kote kuendelea kujenga Ofisi za kisasa zenye hadhi ya Chama chao zikienda sambamba pia na uanzishwaji wa miradi ya kiuchumi kwenye Ofisi hizo.

Balozi Seif aliwatahadharisha wanachama hao wa Chama cha Mapinduzi kujiepusha na tabia za fitna ambazo zikiendekezwa zinaweza kusababisha mpasuko miongoni mwa wanachama wenyewe kitendo ambacho kinaweza kupunguza nguvu za chama hicho kikongwe Nchini.

Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM alielezea matumaini yake kwamba juhudi za ziada zitachukuliwa ili kuona Tawi la CCM la Kijiji cha Boma lililobakiika kati ya Matawi 20 yaliyomo kwenye Jimbo hilo nalo linakamilika kujengwa.

Mbunge huyo wa Jimbo la KitopeBalozi Seif alikabidhi vifaa vya ujenzi kukamilisha hatua ya linta ya Tawi hilo la Kazote ambavyo ni pamoja na Nondo,Matofali, Saruji na Kokoto.

Pia alikabidhi Shilingi Laki 200,000/- za Fundi pamoja na Fedha taslimu kwa Kikundi cha Ushirika cha kuweka na kukopa vyote hivyo vikiwa na thamani ya Shilingi Milioni 1,700,000/-.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top