Shirika la Kimataifa la Mitandao ya Mawasiliano la Microsoft linakusudia kuendesha mradi maalum na Tanzania wa kuwasaidia wanafunzi wa Vyuo Vikuu Nchini Tanzania { Broard Band } katika masomo yao kupitia mfumo wa kisasa wa mtandao wa Internet.

Mfumo huo mpya utamuwezesha kila mwanafunzi wa chuo Kikuu kufikia hatua ya kuwa na Laptop yake itakayoambatana na vifaa vyake vikijumuisha pia huduma za mtandao wa Internet ili kumrahisishia masomo yake.

Makamu wa Rais wa Shirika la Microsoft lenye Makao Makuu yake Mjini Seattle Nchini Marekani Bw. David Tennenhouse alieleza hayo katika kikao cha pamoja kati ya Uongozi wa Shirika lake na Watendaji wa Taasisi za Sayansi, Mawasiliano ya Elimu ya juu Bara na Zanzibar kilichofanyika kwenye ukumbi wa Ofisi ya waziri Mkuu iliyopo ndani ya Jengo la Bunge Mjini Dodoma.

Kikao hicho kilichokuwa chini ya mwenyekiti wake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi kimekuja kufuatia ziara yake aliyoifanya katika Mji wa Seattle Nchini Marekani wiki chache iliyopita ambapo Uongozi wa Microsoft uliahidi kufika Tanzania kwa mazungumzo zaidi ya ushirikiano kati ya pande hizo mbili.

Bwana David Tennenhouse aliwaeleza wajumbe wa kikao hicho kwamba Microsoft tayari imeshatiliana saini Mkataba na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania { Costec } kwa ajili ya kuendesha mradi huo wa Braord Band.

Alifahamisha kwamba awamu ya kwanza ya mpango huo maalum inaanzia kwa wanafunzi wa chuo kikuu cha Dar es salaam na baadaye kuendelea na vyuo vyengine vikuu vya Tanzania.

Kwa Zanzibar mpango huo utajumuisha vyuo vikuu vya SUZA, Tunguu, Chukwani vikiwemo pia chuo cha Ufunsi Mbweni, Chuo cha Elimu ya Afya Mbweni, Chuo cha Uongozi wa Fedha Chwaka pamoja na Chuo cha Kiislamu Mazizini.

Makamu wa Rais wa Shirika hilo la Microsoft alieleza kwamba makubaliano yao mengine ya msingi na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania { Costec } yanahusisha pia mradi wa kusaidia walimu kufundisha mitaala ya Kompyuta { T 21 }.

Akitoa shukrani zake kwa Shirika hilo la Microsoft Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ameupongeza uongozi wa Taasisi hiyo kwa hatua iliyochukuwa katika kipindi kifupi mara tu baada ya ziara yake ya hivi karibuni Nchini Marekani ambapo pia alipata nafasi ya kutembelea Ofisi za Shirika hilo Mjini Seattle.

Balozi Seif alisema Serikali zote mbili ile ya Jamuhuri ya Mungano wa Tanzania na ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia washirika wa maendeleo zimekuwa zikifanya jitihada za kuwajengea mazingira bora ya kitaaluma wanafunzi wake kupitia mfumo mpya wa mawasliano ili wawe na uwezo kamili wa kuhimili mabadiliko ya teknolojia yaliyopo hivi sasa Duniani.

Katika Kikao hicho watendaji wa Taasisi za Mawasiliano, sayansi na Elimu ya Juu ya SMT na SMZ wameuomba uongozi wa shirika hilo la Microsoft kusaidia uanzishwaji wa kituo cha utengenezaji wa mawasiliano { IT Park } pamoja na ulinzi kwenye mitandao kwa ajili ya kuwaepusha watoto na wanafunzi kuingia katika mmong’onyoko wa maadili.

Katika Kikao hichowatendaji wa Taasisi za Mawasilino, Sayansi na Elimu ya juu Tanzania Barana na Zanzibar wameuomba Uongozi wa shirika hilo la Microsoft kusaidia uanzishwaji wa kituo cha utengenezaji wa mawasiliano{ IT Park } pamoja na ulinzi kwenye mitandao kwa ajili ya kuwaepusha watoto na wanafunzi kuingia katika mmong’onyoko wa maadili.

Pia waliomba huduma za misaada na taaluma kwenye E Government, mpango maalum wa ulinzi wa Mkongo wa Taifa pamoja na mradi wa kukusanya vijana kuwashajiisha ili waweze kujiendeleza zaidi kimaisha.

Wakati huo huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alikutana kwa mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Kazi Ulimwenguni { ILO } Bwana Guy Ryder hapo Ofisini kwake Mtaa wa Vuga Mjini Zanzibar.

Katika mazungumao yao Balozi Seif aliushauri Uongozi wa Shirika hilo kuendelea kuiunga mkono Zanzibar na Tanzania kwa ujumla katika harakati zake za kujikwamua katika vikwazo vya kiuchumi likiwemo tatizo la ajira kwa watoto.

Alisema kazi kubwa iliyopo hivi sasa ni kuwajengea mazingira bora ya kitaaluma watoto pamoja na kundi la Vijana kwa lengo la kukabiliana vyema na fursa za ajira ambazo nyingi zinazohitaji kiwango kikubwa cha elimu hupatikana katika Taasisi, Jumuiya na Mashirika Binafsi.

“ Zipo fursa nyingi za ajira hasa katika taasisi, jumuiya na mashirika binafsi lakini mara nyingi kinachojitokeza kwa vijana walio wengi hapa nchini ni kuwa na ufinyu wa taalamu “ Alisisitiza Balozi Seif.

Mapema Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kazi la Kimataifa { ILO } Bwana Guy Ryder alisema mataifa mengi duniani yakiwemo pia yale yaliyoendelea bado yanakabiliwa na changa moto kubwa za ajira hasa kwa Vijana.

Bwana Ryder alisema changamoto hiyo inasababishwa na ukosefu wa taaluma kwa Vijana hao jambo ambalo shirika lake litajitahidi kuona taaluma hiyo inawafikia wahusika hao ili wawe za uwezo wa kujiajiri wenyewe badala ya kutegemea ajira za Serikali.

Mkurugenzi huyo wa Shirika la Kimataifa la Kazi ulimwenguni { ILO } aliipongeza Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na ile ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa ushirikiano mzuri inayotoa kwa shirika hilo hasa katika kukabiliana na ajira za watoto.

Bwana Guy Ryder alimuahidi Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba Shirika hilo litaendelea kusaidia Serikali hizo katika kuona watoto wanaotumikishwa katika kazi mbali mbali wanaachana nazo ili baadaye warejee maskulini.

Mkurugenzi Mkuu huyo wa Shirika la Kimataifa la Kazi Ulimwneguni { ILO } alikuwepo Nchini Tanzzania kwa ziara ya siku Nne kutembelea na kuona Programu na miradi inayosimamiwa pamoja na kufadhiliwa na shirika hilo. 

Othman Khamis Ame 
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top