Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ameondoka Nchini leo jioni kuelekea Johannesburg Afrika ya Kusini kwa ajili ya kuhudhuria sala Maalum ya pamoja ya kuuaga mwili wa Kiongozi mashuhuri Duniani Rais Mstaafu wa nchi hiyo Mzee Nelson Mandela.

Sala hiyo maalum inayotarajiwa kufanyika kesho kwenye uwanja maarufu wa NFP nchini Afrika Kusini inatarajiwa kuhudhuria na Viongozi kutoka zaidi ya nchi sabini Ulimwenguni.

Kwenye uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere Jijini Dar es salaam Balozi Seif aliagwa na Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi Nd. Abdullrahman Kinana pamoja na baadhi ya Viongozi wa Kisiasa na Serikali zote mbili za SMT na SMZ.

Balozi Seif aliyefuatana na Mkewe Mama Asha Suleiman Iddi akimuwakilisha Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr. Ali Mohamed Shein ni miongoni mwa Ujumbe wa Tanzania utaoshiriki tukio hilo ukiongozwa na Rais wa Jamuhuri yaMuungano wa Tanzania Dr. Jakaya Mrisho Kikwete.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar anatarajiwa kurejea Zanzibar kesho kutwa jioni ya Tarehe 11 mwezi Novemba mwaka 2013.

Marehemu Mzee Nelson Madela anayetarajiwa kuzikwa Jumapili ijayo alikuwa Kiongozi shupavu wa Afrika Kusini aliyesimama imara kuongoz mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi uliokuwa ukiendeshwa na Makaburu waliyokuwa wakiitawala nchi hiyo.

Harakati hizo za Mzee Mandela zilipata nguvu kutokana na msaada wa baadhi ya viongozi kadhaa Barani Afrika ambazo hatimaye Makaburu hao wakaamua kumfungulia mashtaka na kufungwa jela kwa takriban miaka 27 katika Kisiwa cha Robin ambacho sasa kimekuwa sehemu kubwa ya Utalii Nchini Afrika Kusini.

Kiongozi huyu ambae ni wa aina yake hapa Duniani alisimama imara kudai haki za watu weusi waliokuwa wakinyanyaswa na kukandamizwa kwa sababu tu ya rangi yao.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Puili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top