Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi mhe. Dr. Emmanuel Nchimbi, amezindua rasmi mpangokazi wa dawati la jinsia na watoto wa jeshi la polisi kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2013 hadi 2016, kwa ajili ya kushughulikia makosa yanayohusu ukatili wa Kijinsia na Watoto. Waziri Nchimbi pia amezindua dawati la jinsia katika kituo cha polisi chang’ombe - Temeke jijini Dar es salaam. Leo ni siku ya pili kati ya mfululizo wa siku 16 za kupinga ukatili na unyanyasaji dhidi ya Mwanamke na Msichana, zilizoanza jumatatu,Novemba 25 mwaka huu.

Uzinduzi wa Mpangokazi huo pamoja na Dawati , unaelezea majukumu ya jeshi la polisi katika mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili wa kijinsia pamoja na unyanysaji wa Watoto. 

Matukio ya ukatili wa kijinsia kwa hapa nchini yamekuwa ni mengi sana,kwa mwaka 2010, taasisi ya utafiti ya Tanzania Health Survey ilitoa makadirio yaliyobainisha kuwa asilimia 45 ya wanawake na wasichana wenye umri wa kati ya miaka 15-49, wameripoti kufanyiwa vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia katika maisha yao. 

Utafiti kuhusu vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia uliozinduliwa na wizara ya maendeleo ya jamii jinsia na watoto mwaka 2011, ulionesha kwamba karibu mtoto mmoja wa kike kati ya watatu na mtoto wa kiume mmoja kati ya saba anakuwa ameshawahi kufanyiwa vitendo vya ukatili wa kijinsia, na zaidi ya 70% ya watoto wa kike na wa kiume wamekumbana na vitendo vya ukatili wa kijinsia wakiwa na umri wa kabla ya miaka 17. Ingawa wengi wao hawasemi na matukio yaliyo mengi hayajawahi kuripotiwa katika vituo vya polisi. 

“Jeshi la polisi Tanzania limejipanga vema katika mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili wa kijinsia na unyanyasaji wa watoto , jeshi linawahakikishia wote kuwa kila kituo cha polisi kitakuwa ni sehemu salama kwa waathirika wa vitendo hivi,” alisema Inspekta Jenerali wa Polisi, Bw Said Mwema.

Kutokana na jukumu la Polisi kushughulikia makosa ya ukatili wa kijinsia na Watoto, kila kituo cha polisi wapo askari waliopewa mafunzo maalumu ya jinsi ya kuwahudumia wahanga wa vitendo hivi kwa usiri na faragha ili kuwafanya watendewa kujisikia huru na salama wanapo toa taarifa/malalamiko yao. 

“Mume wangu alikiri kuninyanyasa na kuahidi kuacha manyanyaso hayo. Sasa tunaishi maisha ya furaha, amani na upendo na ameacha vitendo hivyo na anaendelea kuwalipia watoto wetu karo za shule. Kama mnavyoniona sasa nimependeza kwa kweli,” alisema Mwanahawa.

Mfano mmoja wapo wa kesi ya unyanyasaji wa kijinsia iliyoripotiwa katika dawati la jinsia na watoto Chang’ombe na kushughulikiwa na wataalam wa dawati hilo ni wa bi. Mwanahawa mama wa watoto wawili kutoka Temeke ambaye alikuwa ameolewa kwa miaka 12. Mama huyu alikuwa akinyanyaswa na mumewe ambaye aliacha kuihudumia familia hiyo ikiwa ni pamoja na kukataa kuwasomesha watoto wake ambao walilazimika kuacha shule. 

Baada ya kuishi katika hali hiyo ya manyanyaso kwa takribani miaka mitano, hatimaye aliamua kuomba ushauri kutoka kwa rafiki zake na mmoja wapo alimshauri kwenda kutoa ripoti katika kituo cha polisi chang’ombe kupitia dawati la jinsia na watoto. Hatimaye mume wake aliitwa na waliweza kusuluhishwa na wanaendelea vizuri na maisha yao ya ndoa. 

Malengo ya jeshi la polisi ni kuhakikisha kuwa katika kila kituo cha polisi Tanzania kunatolewa huduma hizi za ukatili wa kijinsia na unyanyasaji wa watoto kwa ubora wa hali ya juu kabisa. 

Umoja wa Mataifa Tanzania kupitia UNICEF kama mratibu wa “Kikundi cha uratibu na polisi dhidi ya ukatili wa kijinsia“, UNFPA na UN WOMEN wanaungana na jeshi la polisi kwa kuunga mkono jitahada hizi za mapambano dhidi ya unyanyasaji na ukatili wa kijinsia kwa wanawake na Watoto.

“Ukatili wa kijinsia na unyanyasaji wa watoto ni ukiukwaji wa haki za binadamu. Sisi sote tunao wajibu wa kuhakikisha kuwa tunatokomeza vitendo hivi. Umoja wa Mataifa(UN) unalipongeza jeshi la polisi kwa hatua walizozichukua kwa mapambano dhidi ya vitendo hivi na kuhakikisha kuwa kunakuwa na madawati ya jinsia na watoto yaliyo kamili katika vituo vyote vya polisi nchini, Umoja wa Mataifa tunajivunia kulisaidia jeshi la polisi katika kutimiza malengo haya”. Alisema Bw. Alberic Kacou mratibu mkaazi wa Umoja wa Mataifa nchini Tanzania.

Mpangokazi wa dawati la jinsia na watoto kwa mwaka 2013-2016 umeandaliwa ili kusaidia jitihada za mapambano ya ukatili wa kijinsia na manyanyaso ya watoto na umeainisha malengo makuu ambayo jeshi la polisi limelenga kuyafikia ndani ya miaka mitatu ijayo.

Jeshi la polisi haliwezi kufikia malengo hayo peke yake hivyo basi Kikundi cha uratibu na ushirika na polisi dhidi ya ukatili wa kijinsia na manyanyaso kwa watoto, chini ya uenyekiti wa jeshi la polisi, washirika toka mashirika yasiyo ya kiserikali NGOs, na wizara husika, idara na wakala mbalimbali, wana wajibu wa kushirikiana na jeshi la polisi katika utekelezaji wa mpangokazi huu ikiwa ni pamoja na mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili na manyanyaso ya kijinsia na watoto

0 comments:

 
Top