Zaidi ya shilingi Milioni Mia Nne na Nne { 204,409,440/- } zinatazamiwa kutumika katika ujenzi wa jengo jipya litakalokuwa na vitega uchumi la Ofisi Kuu ya Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi uliopo hapo katika eneo la Ghimkhana Mjini Zanzibar.

Hayo yamejiri wakati wa Mkutano maalum wa kujitambulisha uliofanyika Ofisi ndogo ya Makamo Makuu ya CCM Iliyopo Mtaa wa Lumumba Mjini Dar es salaam kufuatia kikao cha Baraza Kuu la Umoja wa Vijana wa CCM kilichokutana Mwezi wa sita mwaka huu na kufikia maamuzi ya kuunda Kamati ndogo kwa ajili ya kutafuta fedha za ujenzi wa Ofisi hiyo.

Wajumbe wa Kikao hicho walimpendekeza Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM ambae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi kuwa Mwenyekiti wa Kamati hiyo na Makamu Mwenyekiti wake ni Waziri Mkuu Mstaafu wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Edward Lowasa.

Akitoa Taarifa fupi kwenye Mkutano huo Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM Taifa Mh. Sadifa Juma Khamis alisema Uongozi wa Baraza Kuu la Umoja hupo umefikia hatua hiyo katika azma yake ya kuona Umoja huo unajiendesha kiuchumi na kuepuka mpango wa utegemezi.

Mh. Sadifa alisema asilima kubwa ya watendaji wa Umoja huo hivi sasa wanapata kiwango kikubwa cha mshahara ikilinganishwa na wafanyakazi wa Taasisi nyengine kutokana na Uongozi wa Umoja huo kufanikiwa kuwa na kitega uchumi cha jengo lake la Makao Makuu liliopo Mtaa wa Lumumba Jijini Dar es salaam.

Alisema Umoja huo hivi sasa umekuwa ukipokea sehemu kubwa ya mapato yake kutokana na kodi ya jengo hilo ya zaidi ya Dola za Kimarekani U$ 50,000 sawa na shilingi za Kitanzania Milioni 80,000,000/- na Dola 9,000 ikiwa ni kodi ya Vat kiwango ambacho kimeleta faraja kwa Vijana hao.

Mwenyekiti wa Umoja huo wa Vijana wa CCM Taifa alifahamisha kwamba uamuzi wa Uongozi wa Baraza Kuu la Umoja huo haukufanya makosa kuwapendekeza Balozi Seif na Mh. Edward Lowasa wakielewa kwamba ni viongozi mahiri wenye uwezo wa kushauri, kupendekeza na kusimamia kazi hiyo ngumu inayohitaji nguvu za ziada za pamoja kati ya pande hizo mbili.

“ Hivi sasa tumepata nguvu za ziada katika utaratibu wetu wa kuwalipa mishahara watendaji wetu kutokana na uwekezaji kwenye jengo la Umoja wa Vijana liliopo Mtaa wa Lumumba Jijini Dar es salaam. Mishahara ya watendaji wetu hivi sasa ni mikubwa kiasi kwamba imeleta faraja “. Alifafanua Mwenyekiti huyo wa Umoja wa Vijana wa CCM Taifa Mh. Sadifa.

Naye kwa upande wake mwenyekiti wa Kamati hiyo ya kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa jengo la Ofisi Kuu ya UVCCM Ghimkhana Balozi Seif Ali Iddi aliushukuru Uongozi wa Umoja huo kwa Heshima waliopewa yeye pamoja na Makamu Mwenyekiti wake.

Balozi Seif aliwahakikishia Viongozi wa Umoja huo kwamba watajitahidi katika kuona lengo walilolikusudia kulitekeleza katika uanzishaji wa mradi huo wa ujenzi wa Ofisi Kuu ya UVCCM Zanzibar linafanikiwa vyema.

“ Sisi Baadhi ya Viongozi tumekuwa na tabia ya uzito wa kutoa maamuzi hasa katika masuala yanayohusu maendeleo ya Wananchi. Lakini mimi kwa hili nitakuwa wazi kutoa maamuzi wakati wowote ilimradi huu Mradi unasimama kama ulivyokusudiwa “. Alifafanua Balozi Seif.

Akitoa shukrani zake kwa uteuzi huo Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo ya kutafuta fedha za ujenzi wa Ofisi Kuu ya UVCCM Zanzibar Waziri Mkuu mstaafu wa SMT Mh. Edward Lowasa aliutahadharisha Uongozi wa Umoja huo kuwa makini na kasumba za baadhi ya watu wanaojaribu kuwavunja moyo wananchi na Viongozi wakati wanapoamua kuanzisha miradi yao ya Kiuchumi.

Mh. Lowasa alitolea mfano wa kasumba kama hizo ni ule ujenzi wa Jengo kama hilo la Makao Makuu ya Umoja huo liliopo Lumumba zilizohusishwa na masuala ya rushwa ili kuwakatisha tamaa wasimamizi na Viongozi wa umoja huo.

“ Walisema, wakashawishi na kutia fitina za kutumika rushwa katika ujenzi wa jengo hilo la Makao Makuu ya Umoja wa Vijana wa CCM Lumumba Jijini Dar es salaam, lakini ukweli halisi sasa mnaushuhudia kwa vile nyinyi ndio mnaoendelea kufaidika. Hivyo Mjitahidi kuwa mbali na fitina hizo za Kipuuzi “. Alitahadharisha Makamu Mwenyekiti huyo wa Kamati ndogo Mh. Edward Lowasa.

Pamoja na Kamati Tekelezaji ya Baraza Kuu la Umoja wa Vijana wa CCM kutoa fursa maalum kwa Viongozi hao kuchaguwa idadi na wajumbe wa Kamati hiyo lakini Mkutano huo ulifikia uwamuzi wa kuteua baadhi ya wajumbe watakaounda Kamati hiyo.

Kamati hiyo itakuwa na Wajumbe kumi ambao watatu watatoka Tanzania Bara na watatu kutatoka Zanzibar ambapo mjumbe Mmoja tayari ameshateuliwa ambae ni Mheshimiwa Mohd Raza na Katibu wa Kamati hiyo ameteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu wa UVCCM Zanzibar Chaka Hamdu Shaka.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top