Uingereza imeahidi kuwa itashirikiana na Zanzibar katika kuwajengea uwezo wananchi katika sekta ya mafuta na gesi asilia.

Balozi wa Uingereza nchini Tanzania bibi Dianna Melrose, ameeleza hayo wakati akizungumza na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad, nyumbani kwake Mbweni, nje kidogo ya mji wa Zanzibar.

Balozi Melrose amesema anaamini kuwa Zanzibar ina utajiri mkubwa wa maliasili ikiwemo gesi asilia, na kwamba ili wananchi waweze kunufaika nayo, ni lazima wawe weledi na wataalamu wazalendo katika fani hiyo.

Naye Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad, amemuhakikishi balozi huyo kuwa Zanzibar itashirikiana na Uingereza, na kwamba itafarijika kupata msaada huo wa kitaaluma.

Amesema Zanzibar inahitaji sana wananchi wake kupatiwa taaluma na kujengewa uwezo katika sekta ya mafuta na gesi asilia, haa wakati huu ambapo suala hilo linatarajiwa kutolewa katika orodha ya mambo ya Muungano.

Mazungumzo hayo pia yalimuhusisha Mkuu wa Idara ya Afrika Mashariki na Magharibi, Ofisi ya Mambo ya Nje na Jumuiya ya Madola wa Uingereza bibi Harriet Mathews.

Wakati huo Maalim Seif amekutana na Balozi wa Norway nchini Tanzania bibi Ingunn Klepsvik na kujadiliana juu ya mambo kadhaa yakiwemo Serikali ya Umoja wa Kitaifa na mchakato wa mabadiliko ya Katiba.

Amesema viongozi wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa wanaendelea kushirikiana vizuri katika kutekeleza majukumu ya serikali, ingawaje bado zipo changamoto katika ngazi za chini za uongozi.

Amesema baadhi ya viongozi wa ngazi za chini wakiwemo masheha, bado wanahitaji taaluma zaidi katika kuufahamu muundo huo mpya wa serikali, ili kufikia malengo yaliyowekwa na serikali hiyo, ikiwa ni pamoja na kuwanganisha wananchi.

Kuhusu mchakato wa mabadiliko ya Katiba, Maalim Seif amesema kwa sasa wananchi wanasubiri busara za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais Jakaya Kikwete ambaye ndiye aliyeasisi mchakato huo.

Kwa upande wake balozi Ingunn ameelezea matumaini yake kuwa mchakato wa katiba mpya utamalizika salama na Tanzania itasonga mbele kimaendeleo.

Hata hivyo amesema ipo haja kwa Tanzania kusimamia vyema zoezi hilo, ili kuhakikisha kuwa inapata Katiba itakayokidhi haja, kulingana na mabadiliko ya hali ya kiuchumi, kisiasa na kijamii.

Hassan Hamad, OMKR

0 comments:

 
Top