Uongozi wa Shehia zinazobahatika kupata wawekezaji katika maeneo yao hapa nchini umetakiwa kujenga uhusiano mwema na wawekezaji hao kwa lengo la kupata maendeleo ya haraka yatakayosaidia kustawisha hali za wananachi wao.

Wito huo umetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi katika hafla fupi ya kuzindua Kituo kipya cha Afya katika Kijiji cha Chuini Wilaya ya Magharibi ikiwa ni mwanzoni mwa maadhimisho ya sherehe za kutimia miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964 sawa na nusu Karne.

Balozi Seif alisema Uzoefu unaonyesha kuwa wawekezaji wengi hapa nchini hupendelea kuchangia maendeleo ya wananchi lakini mara nyingi hukatishwa tamaa kwa matumizi mabaya ya misaada wanayoitoa kunaofanywa na baadhi ya Viongozi wa shehia kwa kushirikiana na watendaji wabadhirifu wa Taasisi za Serikali na zile zisizokuwa za Kiserikali.

Alionya kwamba tabia hiyo mbaya inarejesha nyuma maendeleo ya Taifa na wananchi kwa jumla, hivyo hakuna budi kwa wenye hulka hiyo kuachana nayo mara moja.

“ Mara nyingi na baadhi ya maeneo wawekezaji wetu hukatishwa tamaa na udokozi wa baadhi ya wenzetu ambao hujisahau bila ya kuzingatiwa kuwa wawekezaji hao ni wageni wetu tuliyokwenda kuwatafuta ili waje kuwekeza nchini mwetu “. Alifafanua Balozi Seif.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwapongeza wananchi na viongozi wa Shehia ya Chuini kwa kuwepuka matumizi mabaya ya misaada ya wahisani jambo ambalo limesaidia kuwaletea maendeleo ya haraka.

Balozi Seif alifahamisha kwamba wananchi wa Chuini wamefanikia
kuwa na uadilifu mkubwa uliopelekea kulinda na kuheshimu michango inayotolewa na wahisani, wadau na washirika wa maendeleo ndani na nje ya Nchi.

Akizungumzia huduma za afya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ameiasa jamii kujenga utamaduni wa kuvitumia vituo vya afya katika kujipatia huduma bora za afya pamoja na kupata taaluma ya kinga ya maradhi tofauti.


Alisema tabia ya baadhi ya watu wakiumwa kufikiria wamerogwa na kukimbilia kwa waganga wa kienyeji haina tija kwao na kwa kiasi kikubwa inaweza kuhatarisha maisha yao.

“ Tunapougua ni vyema tukakimbilia vituoni ili kutibiwa. Tabia ya kukimbilia kwa waganga wa kienyeji kila mara, bila ya sababu za msingi tuziache mara moja “. Alisisitiza Balozi Seif.

Aliwahakikishia Wananchi wa Shehia ya Chuini kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa upande wake, itajitahidi kuona dawa muhimu kwa ajili ya wananchi hao zinapatikana kituoni hapo pamoja na wafanyakazi wa kutosha.

Kuhusu hali ya ukimwi hapa Nchini Balozi Seif alisema maambukizi ya maradhi hayo imekuwa ikiongezeka kwa kasi badala ya kupungua kama inavyoonekana sehemu nyengine duniani.

Alieleza kwamba Jitihada za Serikali za kupambana na ukimwi hazitaweza kuleta mafanikio bila ya wananchi kushiriki kikamilifu katika vita dhidi ya maambukizi na maradhi hayo ya Ukimwi.

Alitahadharisha kuwa ukimwi hauna tiba, hivyo wananchi wajitahidi kujiepusha na vitendo vyote vinavyochangia kusambaa kwa ukimwi hapa nchini, kama vile uzinifu, ngono zembe pamoja na utumiaji wa dawa za kulevya.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif katika kuunga mkono juhudi za wananchi hao wa Chuini ameahidi kuchangia matofali elfu moja kwa ajili ya kuongeza nguvu za ujenzi wa jengo jipya la Madaktyari wa Kituo hicho cha afya cha Shehia hiyo.

Katika risala yao wananchi hao wa shehia ya Chuini iliyosomwa na katibu wa Kamati ya maendeleo wa shehia hiyo Bibi Narie Mbaraka Kaite alisema Kituo hicho kilichogharimu jumla ya shilingi Milioni 28,000,000/- kitakuwa na huduma zote za msingi.

Bibi Narie alisema uongozi na wananachi wa shehia hiyo hivi sasa wamejikita katika ujenzi wa nyumba ya familia mbili ya daktari ikiwa katika hatua ya msingi ili jamii ya kijiji hicho ifikie hatua ya kupata huduma za afya wakati wote.

Katibu huyo wa kamati ya maendeleo ya shehia ya Chuini kwa niaba ya wananachi na viongozi wa shehia hiyo amewashukuru wafadhili, wahisani na washirika wa maendeleo waliosaidia michango iliyokamilisha ujenzi wa Kituo hicho cha afya.

Naye Mwakilishi wa wahisani na wafadhili wa mradi wa ujenzi wa kituo hicho cha Afya Bwana Paul Jonson na Mkewe Bibi LNY wakitoa salamu zao walisema Kituo hicho kitasaidia ukombozi wa kiafya kwa wananchi walio wengi katika shehia hiyo.

Bwana Paul aliiomba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara inayohusika na masuala ya Afya kukipatria vifaa vya kazi kituo hicho ili kiweze kutoa huduma bora na za kisasa.

Bibi Lny Paul akaisisitiza jamii ya wazanzibari kujenga tabia ya kupenda kulinda na kutunza mazingira ili visiwa vya Zanzibar viendelee kuwa na haiba nzuri.

Kituo cha Afya cha Chuini kitakuwa kikitoa huduma zote za msingi ikiwemo mama wajawazito, watoto, maradhi ya kawaida, ushauri nasaha pamoja namaabara.

Othman Khamis Ame 
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top