Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad, amesema unga mbovu uliopo bandari ya Malindi Zanzibar utakuwa umeondolewa ifikapo tarehe 15 mwezi ujao.

Amesema unga huo upatao tani mia saba umechelewa kuondoshwa na kuangamizwa kutokana na mvutano uliokuwepo baina ya msambazaji na muagiziaji wa unga huo, huku kila mmoja akimtupia jukumu mwenzanke.

Akizungumza na wajumbe wa kamati ya kudumu ya Baraza la Wawakilishi inayosimamia ofisi za viongozi wakuu wa Serikali ofisini kwake Migombani, amesema baada ya mazungumzo ya muda mrefu wahusika hao wamekubaliana kushirikiana na serikali zote mbili katika uangamizwaji wa unga huo.

Hivi karibuni Mawaziri wanaohusika na mazingira wa Zanzibar Mhe. Fatma Abdulhabib Fereji, Dk. Terezya Huvisa wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na Waziri wa Afya Juma Duni Haji, walikutana na kutembelea eneo hilo na kukubaliana juu ya namna ya kuungamiza.

Kwa upande wao wajumbe wa kamati hiyo mpya ya kudumu ya Baraza la Wawakilishi wakiongozwa na Makamu Mwenyekiti Saleh Nassor Juma wamewaomba watendaji wa ofisi hiyo kutoa ushirikiano kwa kamati ili iweze kutekeleza majukumu yake vizuri.

Mapema Makamu wa Kwanza wa Rais aliihakikishia kamati hiyo kuipa ushirikiano wa kutosha, ili iweze kufanya vizuri zaidi kama ilivyokuwa kwa kamati iliyopita.

Hassan Hamad, OMKR

0 comments:

 
Top