Wanafunzi na walimu wa skuli ya Laurete International, wamefanya ziara ya kimasomo katika nyumba za kurekebisha tabia kwa vijana walioamua kuachana na dawa za kulevya “sober houses”, na kusema kuwa ziara hiyo imewapa uwezo mkubwa wa kuelewa athari zitokanazo na matumizi ya dawa za kulevya.

Mkuu wa kitengo cha Sekondari katika skuli hiyo, Mwalimu Moh’d Saleh alisema wamefurahishwa kwa namna wanafunzi wao walivyopokewa na kupatiwa mashirikiano, jambo lililopelekea kuweza kujifunza kwa mafanikio makubwa.

Kufuatia ziara hiyo Mwalimu Mohd ameahidi kuwa walimu na wanafunzi wa skuli hiyo watakuwa mabalozi wazuri wa kuipeleka elimu hiyo katika jamii iliyowazunguka, ili iwe hatua muhimu ya kampeni ya kuwakinga vijana na utumiaji wa dawa za kulevya.

Wanafunzi na walimu hao walipata fursa ya kufanya majadiliano na vijana walioamua kuachana na dawa za kulevya katika nyumba ya vijana hao iliyoko Bububu pamoja na nyumba wanayoishi vijana wa kike iliyoko Kwa Mchina.

Wametoa wito kwa skuli nyengine kutembelea nyumba hizo ili kujifunza kwa vitendo juu ya sababu zilizopelekea vijana hao kujiingiza katika vitendo hivyo, ili waweze kusaidia mapambano dhidi ya dawa za kulevya.

Hivi karibuni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad alizindua kampeni ya mapambano dhidi ya dawa za kulevya maskulini, na kusema kuwa hatua hiyo itasaidia kuwapa vijana wengi elimu inayohusiana na dawa za kulevya, na kufikia azma ya serikali na kutokuwepo kabisa kwa matumizi ya dawa za kulevya Zanzibar.
 
Hassan Hamad, OMKR

0 comments:

 
Top