Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad amesema katika jitihada za kukuza uchumi wa Taifa, serikali inaweka mkazo katika kuziendeleza sekta kuu za kiuchumi zikiwemo Utalii, Kilimo na Uvuvi.

Amesema sekta hizo zina mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa taifa, na kwamba zitaendelea kupewa kipaumbele ili kuhakikisha kuwa uchumi wa Zanzibar unakua hadi kufikia asilimia tisa kwa mwaka.

Akizungumza na ujumbe wa wanafunzi wa Chuo Cha Ulinzi Cha Taifa kilichoko Dar es Salaam waliofika ofisini kwake Migombani kwa ajili ya kuonana nae, Maalim Seif amesema licha ya matatizo ya kiuchumi yanayoikabili dunia mara kwa mara, hali ya uchumi wa Zanzibar inaendelea vizuri ambapo ukuwaji wake ni kati ya asilimia sita hadi saba kwa mwaka.

Amesema athari za kiuchumi zinazotokea duniani zimekuwa zikisambaa katika nchi mbali mbali ikiwemo Zanzibar, lakini athari hizo zimekuwa zikidhibitiwa na serikali kwa kuweka mipango imara ya kudhibiti uchumi wake.

Ameitaja mipango hiyo kuwa ni pamoja kudhibiti mfumko wa thamani ya dola dhidi ya shilingi ya Tanzania, pamoja na kuimarisha sekta za kiuchumi zinazokwenda na wakati kulingana na mabadiliko ya kiuchumi duniani.

Ameielezea sekta ya utalii kama sekta kiongozi kwa uchumi wa Zanzibar baada ya kuporomoka kwa zao la karafuu, na kwamba jitihada zaidi zinafanywa kuiendeleza dhana ya utalii kwa wote, ili kila mwananchi aweze kunufaika moja kwa moja na sekta hiyo.

Maalim Seif amefahamisha kuwa katika kutimiza malengo yake ya kukuza uchumi serikali inaendelea kuwahamasisha wawekezaji wa sekta ya utalii kuja kuwekeza hasa katika ujenzi wa mahoteli yanayofikia hadhi ya “nyota tano”.

Aidha amesema serikali inakusudia kuimarisha ulinzi katika maeneo ya utalii, ili kuhakikisha kuwa watalii wanaokuja wanaishi kwa furaha na amani, na hivyo kuweza kuitangaza Zanzibar kiutalii duniani.

“Sekta ya utalii “is very sensitive”, watalii wanaposikia vurugu kidogo tu hao wanakwenda zao, na hapo kabla baadhi ya mapapasi walikuwa wakiwanyanyasa na wengine kutishia usalama wa watalii, lakini sasa serikali inajipanga kuhakikisha kuwa watalii wanaishi kwa usalama na kufurahia ziara zao nchini mwetu”, alifafanua Maalim Seif.

Amesema chini ya mikakati hiyo serikali inalenga kupokea watalii wapatao laki tano ifikapo mwaka 2015 ambao itakuwa ni ongezeko la asilimia mia moja ya watalii wanaoingia nchi kwa sasa.

Akizungumzia kuhusu kilimo. Makamu wa Kwanza wa Rais amesema serikali inaendelea vyema na mpango wake wa kilimo cha umwagiliaji ambapo wamekuwa wakishirikiana na washirika mbali mbali wa maendeleo ikiwemo Korea ya Kusini ambayo imekubali kusaidia uimarishaji wa miuondombinu ya umwagiliaji.

Ameongeza kuwa wakulima wengi wa Zanzibar wameshajiika kuendeleza kilimo, baada ya serikali kuamua kupunguza gharama za kilimo ikiwa ni pamoja na gharama za kulimia pamoja pembejeo.

Kuhusu Uvuvi Maalim Seif amesema sekta hiyo pia inapaswa kuendelezwa kwa vile inawagusa wananchi wengi wa visiwa vya Unguja na Pemba, na ni miongoni mwa sekta zinazoweza kuwakomboa wananchi kiuchumi.

Amesema kwa sasa wavuvi wanapaswa kujiandaa kwa uvuvi wa bahari kuu, ambao mafanikio yake yatawahamasisha wawekezaji wa mazao ya baharini kuja kuwekeza katika sekta hiyo na kuongeza pato la Taifa.

Nae kiongozi wa ujumbe wa wanafunzi hao wanaojifunza masuala ya kiuchumi Brigedia General R. S. Laswai ameelezea matumaini yake ya kuendeleza kozi hiyo kwa mafanikio kufutia maelekezo na mashirikiano wanayoyapata kutoka kwa viongozi wa serikali.

Hii ni kozi ya pili kuendeshwa na chuo hicho tangu kuanzishwa rasmi mwezi Septemba mwaka jana, ambapo kozi ya mwanzo ilihusu mafunzo ya kijamii “Social studies” na zimekuwa zikiwashirikisha watendaji wa taasisi tofauti zikiwemo vikosi vya ulinzi Bara na Zanzibar pamoja na taasisi za kijamii. 

Hassan Hamad (OMKR)

0 comments:

 
Top