Vyombo vya Habari Nchini bado vinapaswa kutumiwa  Kisayansi katika kutoa Elimu juu ya uhamasishaji wa umuhimu wa Zoezi la Sensa ya Watu na Makaazi inayotarajiwa kufanyika Nchini kote Usiku wa Kuamkia Tarehe 26 Agosti mwaka 2012. Ushauri huo umetolewa  na Wajumbe wa Kamati ya Taifa ya Sensa ya Watu na Makaazi katika Kikao chao cha Tatu kilichofanyika  kwenye ukumbi wa Mikutano wa Wizara ya Nchi Ofisi ya Waziri MkuuTawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Kikao hicho kilichoshirikisha  Wajumbe wa Pande zote mbili za Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ambao ni Mawaziri na Watendaji wa Kamati ya Sensa  kiliongozwa na Mwenyekiti wake Waziri Mkuu   Mh. Mizengo Pinda  akiwa na Mwenyekiti Mwenza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi. Wajumbe hao walisema  baadhi ya vyombo vya Habari Watendaji wake  hawajawa na Uzalendo katika utowaji wa Elimu ya Sensa na badala yake  hutumia njia ya kupotosha. Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Fedha,  Uchumi na Mipango ya Maendeleo  Zanzibar Mh. Omar Yussuf Mzee alisisitiza kwamba Wana Habari ni vyema wakawaongoza Wananchi hasa Vijijini katika kuwapatia Elimu hii. Alishauri kutumiwa zaidi Redio za Jamii pamoja na Zile za masafa mafupi { yaani F.M. } katika kutoa Ujumbe wa Elimu ya Sensa kwa vile zimekuwa na wasikilizaji wengi zaidi.  Kwa upande wake Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Zanzibar Mh. Said Ali Mbarouk ambaye ni Mjumbe Mpya katika Kamati hiyo kufuatia mabadiliko ya Uteuzi wa Rais wa Zanzibar ya hivi karibuni aliomba Vyombo vya Habari viwezeshwe zaidi ili kuwa na Uwezo wa kufanya vipindi mbali mbali vya uhamasishaji Jami.   Mh. Said alisema  mfumo na Taratibu za kuvitumia vyombo hivyo ni muhimu na wa msingi ikizingatia kwamba asilimia kubwa ya Jamii hivi sasa  hutumia vyombo vya Habari katika kupata Elimu na Habari mbali mbali.  Waziri anayeshughulikia Ajira, Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi na Ushirika Mh. Haroun Ali Suleiman alitoa wazo la kutumiwa kwa Wanafunzi wa Skuli za Sekondari katika kufikisha ujmbe na Taaluma ya Sensa kwa Jamii kwenye Maeneoyao.  Waziri Haroun alisema hatua hiyo inafaa kwenda sambamba na ushirikishwaji wa Watu Maarufu , Waheshimiwa pamoja na Machifu katika kusambaza Elimu hiyo muhimu kwa Taifa.    Akitoa baadhi ya ufafanuzi wa hoja ya baadhi ya wajumbe wa Kikao hicho Kamishna wa Sensa Mh. Amina Mrisho Said  alisema Kamati hiyo inapendelea kuwa na Maswali  machache kwenye zoezi la  hesabu ya Watu na Makaazi. Mh. Amina Mrisho alisema  hatua hii  hupunguza matumizi yasiyo ya lazima kigezo cha Takwimu ambacho hutumiwa pia na Umoja wa Mataifa kwa kuzitaka Nchi Wanachama  wa Umoja huo kutumia mfumo huo.  Katika Nasaha zake Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Sensa Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamuhuri yha Muungano wa Tanzania Mh. Mizengo Pinda  ameshauri  kutumiwa Ziara za Viongozi Wilayani na Mikoani katika kupeleka Elimu na Ujumbe wa Sensa.  Mh. Pinda alieleza kuwa kutumiwa kwa utaratibu huo kutawezesha kufikisha  kwa haraka Taaluma hiyo kwa vile ziara hizo hukusanyisha Wananchi walio wengi.

0 comments:

 
Top