Rasimu ya Muswada wa Sheria ya Mfuko wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar ni hatua muhimu katika kuweka taratibu zitakazoliwezesha Baraza hilo kutekeleza  kazi zake kwa ufanisi mkubwa  kwa mujibu wa matakwa  ya Katiba ya Zanzibar.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi  Seif  Ali Iddi alieleza hayo katika semina ya Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar kuhusu Rasimu ya Muswada wa Sheria ya Mfuko wa Baraza la Wawakilishi pamoja na ile ya Sensa ya Watu na Makaazi ya Mwaka 2012 iliyofanyika hapo Zanzibar Beach Resort Mazizini Mjini Zanzibar.
Balozi Seif alisema Sheria ya Mfuko wa Baraza endapo utaanzishwa utaliwezesha Baraza la Wawakilishi kuwa huru katika utendaji wake na kuliondolea utaratibu wa kuomba omba pale linapohitaji fedha kwa ajili ya kutekeleza majukumu yake.
Balozi Seif alisema kutokana na majukumu hayo ni dhahiri panahitajika kuwepo kwa utaratibu mzuri utakaoliwezesha Baraza hilo kufanya kazi zake ambao ni kuwa na uhuru  kifedha.
“ Kidemokrasia Baraza la kutunga Sheria halitakiwi kuwa omba omba pale alinapohitaji fedha kwa ajili ya kuyetekelza majukumu yake kikatiba, vyenginevyo linaweza kuwa Baraza butu lisilokuwa na makali yoyote ”. Alisisitiza Balozi Seif.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisema Mkutano wa Chama cha Mabunge ya Jumuiya ya Madola uliofanyika Zanzibar Mnamo mwaka 2005 ulijadili nanma ya kuyajengea uwezo wa uhuru wa mambo ya Kifedha Mabunge Wanachama Ikiwemo Tanzania .
Alisema baadhi ya Mabunge yamanza kutekeleza maazimio ya Mkutnao huo ikiwemo Tanzania na Baraza la Wawakilishi Zanzibar liko katika hatua ya kutekeleza Maazimio ya Mkutano huo.
Akizungumzia kuhusu Sensa ya Watu na Makazi Balozi Seif aliwaomba Wawakilishi kuwa Mabalozi wa kufikisha taaluma kwa Wananchi kuhusu umuhimu wa zoezi ya kuhesabiwa wakati utakapowadia.
Alisema kwa upande wa  maandalizi ya kutenga maeneo ya kuhesabu watu ili kurahisisha kazi za kuhesabu watu Zanzibar imeshamaliza kwa Wilaya zote kumi.
Sensa ya Watu na Makazi inatarajia kufanyika Nchini kote Tanzania Tarahe 26 Agosti mwaka 2012.
Wakichangia Mada ya Rasimu ya Mswada wa Mfuko wa Baraza la Wawakilishi baadhi ya Wawakilishi waliwashauri watendaji wa Serikali kujenga Utamaduni wa kuheshimu Mihimili mitatu inayoendesha Nchi.
Walisema Rasim iliyotolewa bado haijakidhi hata kidogo matakwa yaliyokusidiwa.
Wawakilishi hao walitahadharisha kwamba baadhi yavipengele vya Rasimu hiyo vinaashiria muelekeo wa mgongano kati ya Baraza la Wawakilshi  na Serikali  ambavyo vyote ni Mihimili mitatu inayoendesha Nchi ikiwemo Mahkama.
“ Si vyema ukawepo kati ya Baraza la Serikali. Mihimili hii hii inapaswa iheshimiwe na kuwa na Uhuru wa kufanya kazi zao katika misingi ya Sheria na Kanuni zilizowekwa  ”. Alitahadharisha Mh. Asha Bakari Makame Mwaklishi wa Viti Maalum.
Wawakilishi hao waliomba rasim hiyo irejeshwe Serikalini kwa maarekebisho zaidi ya msingi na si vibaya ukachelewa kupelekwa Barazani ili kupata wasaa wa marekebisho hayo.
Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

0 comments:

 
Top