A. UTANGULIZI
1. Mheshimiwa Spika, kufuatia taarifa iliyowasilishwa leo ndani ya Bunge lako tukufu na Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako tukufu likubali kupokea, kujadili na kupitisha Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka 2014/2015.
2. Mheshimiwa Spika, ninasimama mbele ya Bunge lako tukufu kwa mara ya kwanza toka niteuliwe na Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, kuwa Waziri wa Katiba na Sheria. Kwa hiyo kabla ya kuwasilisha Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka 2014/2015, naomba nichukue fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kunipa heshima hii kubwa. Ninapenda kumhakikishia Mheshimiwa Rais na Watanzania wenzangu wote kwamba nitafanya kazi kwa bidii, uadilifu na kujituma kwa uwezo wangu wote.
3. Mheshimiwa Spika, naomba sasa uniruhusu nitoe pole zangu za dhati kwako kufuatia vifo vya wabunge mahiri, Mheshimiwa Dkt. William Augustao Mgimwa, aliyekuwa Mbunge wa jimbo la Kalenga na Waziri wa Fedha wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania; na Mheshimiwa Saidi Ramadhani Bwanamdogo, aliyekuwa Mbunge wa jimbo la Chalinze. Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema peponi.
4. Mheshimiwa Spika, ninayo furaha kuwapongeza wabunge wenzangu ambao ni wapya, Mheshimiwa Yusuf Salim Hussein, kwa kuchaguliwa kuwa Mbunge wa jimbo la Chambani; Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa kwa kuchaguliwa kuwa Mbunge wa jimbo la Kalenga; na Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Kikwete kwa kuchaguliwa kuwa Mbunge wa jimbo la Chalinze. Ninawatakia kheri na mafanikio katika majukumu yao mapya.
5. Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee natoa pongezi na shukurani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda, Mbunge wa jimbo la Mpanda Mashariki, na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, kwa hotuba yake ambayo imetoa mwelekeo wa ujumla wa shughuli za Serikali kwa mwaka wa fedha 2014/2015.
6. Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii pia kutoa shukurani zetu za dhati kwa Waheshimiwa Wajumbe wote wa Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala chini ya uongozi mahiri wa Mwenyekiti wake Mheshimiwa William Mganga Ngeleja, Mbunge wa jimbo la Sengerema. Maoni, ushauri na maelekezo yao yameiwezesha Wizara yangu kutekeleza majukumu yake kwa mafanikio. Tutaendelea kuzingatia ushauri wa Kamati hii wakati tukitekeleza malengo yetu kwa mwaka huu wa fedha na katika siku zijazo kwa ujumla.
7. Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kumpongeza sana Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Mheshimiwa Jaji Joseph Sinde Warioba na Makamu wake Mheshimiwa Jaji Augustino Ramadhani kwa kuiongoza vema Tume hiyo. Ninawapongeza pia wajumbe wote kwa kazi kubwa waliyoifanya. Rasimu ya Katiba waliyoiwasilisha imetuwekea msingi mzuri wa kujadili uandishi wa Katiba mpya, jambo ambalo lina mchango wa pekee katika kujenga mustakabali wa taifa letu. Ni matumaini yangu kwamba tutapata Katiba bora itakayotuongoza kwa miaka mingi ijayo, itakayoimarisha umoja wetu na itakayoleta utangamano wa kitaifa na ustawi wa nchi yetu.
B. MUUNDO NA MAJUKUMU YA WIZARA
8. Mheshimiwa Spika, Wizara ya Katiba na Sheria inajumuisha Mahakama ya Tanzania, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Tume ya Kurekebisha Sheria, Tume ya Utumishi wa Mahakama, Wakala wa Usajili, Ufilisi, na Udhamini (RITA), Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo, na Chuo cha Uongozi wa Mahakama. Kwa pamoja taasisi hizi ndizo zinazotekeleza majukumu ya Wizara kama yalivyoainishwa kwenye Tangazo la Serikali Namba20 la mwaka 2010.
9. Mheshimiwa Spika, Wizara ya Katiba na Sheria kwa kuzingatia dira yake ya upatikanaji haki kwa watu wote na kwa wakati, inasimamia na kutekeleza majukumu yafuatayo: masuala ya kikatiba na kisheria; shughuli za uendeshaji wa mashauri na utoaji haki; utekelezaji wa haki za binadamu na utawala bora; shughuli za utafiti, urekebu na uandishi wa sheria; kuishauri na kuiwakilisha Serikali katika masuala ya kisheria ndani na nje ya nchi; shughuli za usajili, ufilisi na udhamini; kuratibu taasisi za mafunzo zilizo chini yake na kusimamia maslahi na maendeleo ya watumishi.
C. MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA BAJETI KWA MWAKA 2013/2014
10. Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/2014 Wizara yangu ilitekeleza malengo iliyojiwekea ambayo ni yafuatayo: kuratibu mchakato wa mabadiliko ya Katiba; kusikiliza na kuendesha mashauri nchini; kusimamia masuala ya haki za binadamu na utawala bora; kutoa huduma za kisheria; kuhakiki na kushiriki majadiliano ya mikataba mbalimbali; uandishi wa sheria na hati za Serikali; kufanya tafiti na tafsiri ya sheria; kuendesha shughuli za usajili, ufilisi na udhamini; na kuratibu mafunzo ya uanasheria kwa vitendo na uongozi wa Mahakama. Pia, Wizara iliboresha miundombinu ya utoaji haki; ilitoa elimu na habari kuhusu upatikanaji haki kwa jamii; iliratibu shughuli za maboresho ya Sekta ya Sheria na kuimarisha usimamizi na uwajibikaji katika matumizi ya rasilimaliza umma. Utekelezaji wa majukumu hayo umefanyika kwa mafanikio na viwango mbalimbali vya utekelezaji.
Kuratibu Mchakato wa Mabadiliko ya Katiba
11. Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha kwamba nchi yetu inakuwa na mfumo imara wa sheria unaozingatia mahitaji ya wakati tulionao, Wizara ya Katiba na Sheria ilisimamia na kuratibu mchakato wa kihistoria wa kuandika Katiba. Tofauti na michakato miwili iliyopita (mwaka 1965 na mwaka 1977), safari hii mchakato wa kuandika Katiba ulihusisha watu wengi zaidi. Wananchi wameshiriki moja kwa moja kwa kutoa maoni yao mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba au kwa maandishi. Hali kadhalika watashiriki kufanya uamuzi wa mwisho kuhusu Katiba inayopendekezwa kupitia kura ya maoni. Aidha, wananchi walipata fursa ya kupendekeza majina ambayo Mheshimiwa Rais aliyazingatia katika kufanya uteuzi wa wajumbe wa Tume.
12. Mheshimiwa Spika, Tume hii ilifanya kazi ya kukusanya maoni kutoka kwa wananchi moja kwa moja na kupitia mabaraza ya Katiba ya wilaya na ya kitaasisi. Baada ya zoezi hili Tume iliandaa Ripoti iliyojumuisha Rasimu ya Katiba. Ripoti hiyo iliwasilishwa kwa Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, na Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi mnamo tarehe 30 Desemba, 2013.
13. Mheshimiwa Spika, baada ya kupokea Ripoti ya Tume, Mheshimiwa Rais aliitisha Bunge Maalum ambalo lilianza kazi rasmi kwa kupokea Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Mheshimiwa Jaji Joseph Sinde Warioba tarehe 18 Machi, 2014. Tume ilihitimisha kazi zake na kuvunjwa rasmi kwa Tangazo la Serikali Namba 81 la tarehe 21 Machi, 2014.
14. Mheshimiwa Spika, Bunge Maalum lilizinduliwa rasmi na Mheshimiwa Rais tarehe 21 Machi 2014. Hadi sasa Bunge Maalum limefanya kazi ya kuandaa Kanuni za kusimamia uendeshaji wa shughuli zake za kila siku. Aidha, Bunge Maalum limejadili Sura ya Kwanza na Sura ya Sita ya Rasimu ya Katiba kama hatua za awali za uchambuzi wa Rasimu hiyo.
Kuimarisha Haki za Binadamu na Utawala Bora
15. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2013/2014 Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imetoa elimu kwa umma katika masuala ya haki za binadamu na utawala bora. Elimu iliyotolewa ilihusu sheria za ardhi na umiliki wa mali, ambapo wananchi 8,529 kutoka katika kata 69 na Shehia 7 walifikiwa. Pamoja na kutoa elimu, Tume ilipokea malalamiko 923 ya aina mbalimbali katika kipindi hicho yakiwemo yale yanayohusu migogoro ya ardhi. Kati ya malalamiko hayo, malalamiko 324 yalishughulikiwa na kutolewa uamuzi.
16. Mheshimiwa Spika, Tume iliandaa Mwongozo wa Utawala Bora wenye lengo la kukuza uelewa katika eneo hili. Jumla ya nakala 25,000 za Mwongozo huo zilisambazwa kwa watendaji wa ngazi za vijiji na kata ili waweze kuzingatia misingi ya utawala bora na haki za binadamu wakati wanapotekeleza majukumu yao.
17. Mheshimiwa Spika, hadhi ya Tanzania kuhusu haki za binadamu imeendelea kuwa nzuri ndani na nje ya nchi yetu. Ni wajibu wa Wizara yangu kukuza na kuendeleza mafanikio yaliyokwishapatikana. Wizara imekamilisha Rasimu ya Taarifa ya utekelezaji wa masuala ya haki za binadamu hapa nchini ambayo itawasilishwa kwenye Kamisheni ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu. Taarifa hiyo inaeleza namna ambavyo Serikali yetu inatekeleza mikataba mbalimbali ya kitaifa, kikanda na kimataifa katika kukuza na kulinda haki hizo.
18. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha 2013/2014, Wizara iliandaa Mpango Kazi wa Kitaifa wa Haki za Binadamu (2013–2017) uliozinduliwa na Makamu wa Rais Mheshimiwa, Dkt. Mohamed Gharib Bilal, tarehe 10 Desemba, 2013. Wizara yangu ina wajibu wa kusimamia na kuratibu utekelezaji wa Mpango Kazi huu katika taasisi kadhaa za umma na za kijamii. Kupitia Mpango huu wadau mbalimbali watapata fursa ya kujadili na kutekeleza masuala ya haki za binadamu. Pia ni fursa kwa Wizara kuimarisha usimamizi na ufuatiliaji wa masuala mbalimbali yanayohusu haki za binadamu na utawala bora.
19. Mheshimiwa Spika, uzinduzi huo ulikwenda sambamba na uzinduzi wa Mpango Mkakati wa Miaka Mitano wa Haki za Watoto (2013-2017). Mpango huo uliandaliwa kutokana na tafiti mbili zilizofanywa juu ya upatikanaji haki kwa watoto wanaokutana na mkono wa sheria na hali ya watoto wanaokinzana na sheria. Matokeo ya tafiti hizo yaliwezesha kubaini vipaumbele vya kimkakati ndani ya mkakati wenyewe na hatua madhubuti zinazopaswa kuchukuliwa katika kipindi cha miaka mitano ya utekelezaji wa Mpango huo.
20. Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inaratibu shughuli za Kamati ya Kitaifa ya Kuzuia Mauaji ya Kimbari iliyoundwa chini ya Itifaki ya nchi za Maziwa Makuu ya kuzuia mauaji ya kimbari. Kamati hii ina jukumu la kujenga uelewa na kuishauri Serikali juu ya viashiria vinavyoweza kuathiri amani na kusababisha vitendo vya ukatili kwa binadamu. Katika kipindi cha mwaka 2013/2014, pamoja na kutoa elimu kwa umma juu ya masuala ya amani kupitia redio na luninga, Wizara imewajengea uwezo viongozi wa dini na madhehebu mbalimbali katika kulinda amani katika mikoa ya Arusha, Mbeya, Mwanza, Mjini Magharibi, Morogoro na Tanga. Katika mikoa hii, viongozi wa dini waliunda Kamati za amani zenye wajumbe kutoka dini na madhehebu mbalimbali. Kamati hizi zina jukumu la kuhakikisha amani inadumishwa katika mikoa hiyo.
21. Mheshimiwa Spika, katika uendeshaji wa shughuli zake, azma ya Serikali ni kuongeza uwazi katika ngazi zote za utendaji. Ili kufikia lengo hilo Serikali ilijiunga na Mpango wa Kimataifa wa uendeshaji wa Serikali kwa Uwazi (Open Government Partnership) mwaka 2011. Tamko la Tanzania katika kutelekeza matakwa ya ubia huu ni kuweka mazingira ya upatikanaji wa taarifa kuhusu shughuli zinazofanywa na Serikali. Wizara yangu iliandaa Rasimu ya Waraka wa Baraza la Mawaziri wa mapendekezo ya kutunga sheria ya haki ya kupata taarifa kutoka katika taasisi za umma kwa lengo la kuongeza uwazi na uwajibikaji wa Serikali.
22. Mheshimiwa Spika, pamoja na hali nzuri ya utawala bora na kuzingatiwa kwa haki za binadamu katika nchi yetu, hivi karibuni kumekuwa na tuhuma nzito kuhusu ukiukwaji wa haki za binadamu. Tuhuma hizo zilitokana na utekelezaji wa “Operesheni Tokomeza” ambayo ililenga kuwasaka na kuwafikisha kwenye vyombo vya Sheria watu wote waliokuwa wanajihusisha na vitendo vya ujangili katika hifadhi za taifa na mapori tengefu. Kwa kuzingatia uzito wa tuhuma hizo Mheshimiwa Rais ameunda Tume ya Uchunguzi chini ya Sheria inayohusu uundwaji wa Tume za Uchunguzi (Commissions of Inquiry Act, Cap. 32). Kuundwa kwa Tume hiyo kulitangazwa katika Gazeti la Serikali na. 131 la tarehe 2 Mei, 2014. Tume hiyo yenye makamishna watatu (3) imepewa hadidu za rejea ambazo ni:
(i) Kuchunguza namna Operesheni Tokomeza ilivyofanyika;
(ii) Kuchunguza kama maofisa walioendesha Operesheni hiyo walifuata sheria, taratibu na hadidu za rejea walizopewa;
(iii) Kuchunguza endapo maofisa walioendesha Operesheni hiyo walivunja sheria, taratibu na hadidu za rejea zilizotolewa;
(iv) Kuchunguza kama kuna watu waliovunja sheria wakati wa Operesheni hiyo na kuona kama hatua walizochukuliwa wenyewe au mali zao zilikuwa sahihi;
(v) Kushauri hatua zinazopaswa kuchukuliwa kwa mtu yeyote aliyevunja sheria, taratibu na kwenda kinyume na hadidu za rejea zilizokuwepo katika kutekeleza Operesheni hiyo;
(vi) Kushauri mambo yanayopaswa kuzingatiwa wakati wa kuandaa Operesheni nyingine kama hiyo ili mambo yaliyojitokeza katika Operesheni hii yasijirudie.
Kusikiliza na kuendesha mashauri nchini
23. Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia Dira ya upatikanaji haki kwa watu wote na kwa wakati,Wizara yangu imeongeza kasi ya kuendesha na kusikiliza mashauri yaliyosajiliwa Mahakamani. Kasi hiyo imetokana na mikakati mbalimbali na malengo mahsusi ambayo Mahakama ya Tanzania imejiwekea ya kusikiliza mashauri kwa ngazi zote za Mahakama. Utaratibu huu unaweka wastani wa idadi ya mashauri yatakayosikilizwa na kila ngazi ya Mahakama kwa kila mwaka. Katika Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu lengo ni kumaliza mashauri mapya ndani ya miezi 24, Mahakama ya Hakimu Mkazi katika muda usiozidi miezi 18 na Mahakama ya Mwanzo kumaliza mashauri mapya ndani ya miezi 12.
24. Mheshimiwa Spika, mkakati huu umesaidia kupunguza mlundikano wa mashauri kwa kiasi kikubwa ambapo hadi kufikia Desemba, 2012 Mahakama ya Tanzania ilikuwa na jumla ya mashauri 114,278 yaliyohusu masuala ya madai, jinai na ardhi. Katika mwaka 2013 Mahakama ilisajili mashauri mapya ya aina hiyo 168,068 na kufanya idadi ya mashauri yaliyokuwepo kufikia 282,346. Hadi mwezi Desemba 2013 jumla ya mashauri 182,237 yalisikilizwa na kutolewa uamuzi, sawa na asilimia 65 ya mashauri yote yaliyosajiliwa mahakamani. Mashauri yaliyobaki Mahakamani ni 100,109.(Kiambatisho “A”).
25. Mheshimiwa Spika, mkakati huu umeanza kwa mafanikio ambapo hivi sasa mashauri mengi yanayosajiliwa Mahakamani yamekuwa yakimalizika katika kipindi kisichozidi miaka miwili. Wizara yangu itaendelea kubuni njia mbalimbali zitakazosaidia kuondokana na tatizo la mlundikano wa mashauri na ambalo linaathiri utoaji haki.
26. Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inaratibu na kusimamia utekelezaji wa mpango wa kutenganisha kazi ya upelelezi wa jinai na uendeshaji wa mashtaka. Baadhi ya mafanikio yaliyopatikana hadi sasa ni pamoja na kupungua kwa tuhuma za wananchi za kubambikiziwa kesi katika Mahakama ambazo Mawakili wa Serikali wanaendesha mashauri ya jinai na kupungua kwa idadi ya wafungwa na mahabusu magerezani. Kabla ya kuanza kwa mpango huu, mwaka 2007 kulikuwa na wafungwa 22,622 na mahabusu 20,210. Tangu wakati huo idadi ya wafungwa na mahabusu imekuwa ikipungua kadri Wizara inavyoendelea kueneza utekelezaji wa mpango huu katika mikoa na wilaya mbalimbali. Katika mwaka wa fedha wa 2013/2014 idadi ya wafungwa ilipungua kutoka 16,869 mwezi Juni 2013 hadi wafungwa 15,659 mwezi Machi 2014 na idadi ya mahabusu ilipungua kutoka 17,046 mwezi Juni 2013 na kufikia mahabusu 16,647 mwezi Machi 2014.
27. Mheshimiwa Spika, Kurugenzi ya Mashtaka pamoja na Mahakama ya Tanzania zimeanza kutekeleza utaratibu maalum wa kukamilisha usikilizaji wa mashauri 28 ya dawa za kulevya yaliyosajiliwa Mahakama Kuu. Mashauri haya yamepangwa kusikilizwa katika kikao maalumu cha Mahakama Kuu kitakachofanyika kuanzia mwezi Juni 2014. Mashauri 110 yapo Mahakama za wilaya na mikoa kwa hatua za awali za kuyaandaa ili yahamishiwe Mahakama Kuu kwa ajili ya kusikilizwa. Mashauri haya ni yale yenye thamani inayoanzia shilingi milioni kumi na kuendelea.
28. Mheshimiwa Spika, Wizara inaendelea na utekelezaji wa mkakati maalumu wa kusikiliza mashauri 9 ya jinai ya wizi wa shilingi bilioni 29.8 zilizokuwa katika akaunti ya madeni ya nje (external payments arrears account - EPA) iliyokuwa Benki Kuu. Hivi sasa Kurugenzi ya Mashtaka inaendesha jumla ya mashauri 14 yanayotokana na makosa ya utakatishaji wa fedha kiasi cha shilingi bilioni 56 zilizopatikana kwa njia ya uhalifu, na mashauri mengine 70 ya kukutwa na nyara za Serikali,zenye thamani ya shilingi bilioni 45 kinyume cha sheria.
29. Mheshimiwa Spika, kufikia mwezi Aprili 2014 kulikuwa na jumla ya majalada 404 ya uchunguzi wa makosa mbalimbali ya rushwa yaliyowasilishwa katika Kurugenzi ya Mashtaka kutoka TAKUKURU. Kati ya hayo, majalada 202 yaliandaliwa hati za mashtaka, 103 yalirudishwa TAKUKURU kwa ajili ya uchunguzi zaidi, na majalada 98 yanaendelea kufanyiwa uchambuzi.
30. Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/2014 Wizara ikishirikiana na taasisi mbalimbali iliongeza jitihada zake za kukabiliana na vitendo viovu wanavyofanyiwa watu wenye ulemavu wa ngozi. Jitihada hizi zimechangia kiasi kikubwa kupungua kwa idadi ya matukio ya aina hii katika kipindi cha Julai 2013 hadi Mei 2014, ambapo hakuna tukio lolote lililoripotiwa Polisi. Hali hii ni tofauti na mwaka wa fedha 2012/2013 ambapo matukio matatu yaliripotiwa Polisi. Hivi sasa Wizara yangu inaendelea na mashauri 9 ya aina hiyo yanayotokana na matukio ya miaka ya nyuma.
31. Mheshimiwa Spika, kuhusu mashauri ya ukiukwaji wa Haki za Binadamu, Wizara yangu iliendesha mashauri 6 kwenye Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu iliyopo Arusha. Mashauri haya yanajumuisha mashauri 4 mapya ambayo bado yanaendelea na mashauri 2 ambayo yametupiliwa mbali na Mahakama hiyo kutokana na waombaji kutotimiza matakwa ya sheria.
32. Mheshimiwa Spika, jumla ya mashauri ya madai ambayo Serikali ilishitaki au kushitakiwa, na yale yanayohusu Katiba yaliyokuwa Mahakama Kuu, Mahakama ya Rufani na katika mabaraza ya usuluhishi (mediation and arbitration) katika kipindi cha Julai 2013 hadi Aprili 2014 ni 750. Kati ya hayo mashauri yaliyosikilizwa na kutolewa uamuzi ni 89. Serikali ilishinda mashauri 77 yenye thamani ya Shilingi 2,216,502,356,629 na kuokoa kiasi hicho cha fedha. Serikali ilishindwa mashauri 12 yenye thamani ya Shilingi 25,986,416,661.
33. Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada za Serikali za kupambana na vitendo vya uhalifu, bado kumekuwepo na matukio ambayo baadhi ya watu wamejipatia mali kinyume cha sheria. Kwa kutambua hilo, Wizara yangu imekuwa ikitenga fedha kwenye mipango yake ya mwaka kwa ajili ya kujenga uwezo wa Kitengo cha utaifishaji na urejeshaji wa mali zilizopatikana kwa njia ya uhalifu(Assets Recovery and Forfeiture Section). Kati ya Julai 2013 na Machi 2014, Mahakama iliamuru kurejeshwa Serikalini jumla ya mali na fedha zinazofikia thamani ya zaidi ya shilingi milioni 233 baada ya watuhumiwa kutiwa hatiani.
Kuimarisha utoaji wa huduma za kisheria
34. Mheshimiwa Spika, Wizara imeboresha mazingira ya upatikanaji haki kwa wananchi ikitambua kuwa uwakilishi mbele ya vyombo vya sheria ni haki ya msingi. Katika kipindi cha Julai 2013 hadi Machi 2014 Wizara iliandaa Rasimu ya Waraka wa Kutunga Sheria ya Huduma ya Msaada wa Kisheria ili kuwapa fursa wananchi kupata msaada wa kisheria. Rasimu ya Waraka huo imewasilishwa Serikalini. Sheria hii itakapotungwa.